Polisi mkoani Tanga imesema imefanikiwa kupata bunduki aina ya SMG,
ikiwa na risasi 20 ndani ya mapango ya Majimoto katika eneo la Amboni,
inayodaiwa ilikuwa ikitumiwa na wahalifu waliorushiana risasi na askari mwishoni mwa wiki.
Aidha, imesema inashikilia watu kadhaa akiwemo aliyesababisha kupatikana
kwa bunduki hiyo.
Baadhi ya watu wanaendelea kuhojiwa, kupata taarifa kwa lengo la
kukamata waliopora silaha kwa askari na
kurushiana risasi kwenye mapango hayo.
Kupatikana kwa silaha hiyo, kunafuatia msako maalumu uliodumu kwa siku
nne sasa, uliolenga kusaka silaha na wahalifu wanaodaiwa kujificha ndani ya
mapango ya mawe yaliyopo Amboni, nje kidogo ya mji wa Tanga.
Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi la Polisi, Paul Chagonja alitoa taarifa hiyo jana kwa waandishi wa
habari mjini hapa.
Alisema mafanikio hayo, yametokana na subira ya wakazi wa Tanga na
ushirikiano mkubwa wanaoendelea kuuonesha kwa Polisi inayoshirikiana na vikosi vingine vya ulinzi na usalama, kufanya
operesheni ya pamoja kwenye eneo hilo.
“Kutokana na taarifa kutoka kwa wananchi Februari 16 mwaka huu katika
kitongoji cha la ‘Kona Z’ kilichopo Amboni, tulifanikiwa kumkamata mtu mmoja
ambaye kwa sasa sitamtaja jina kwa sababu upelelezi unaendelea, tulimhoji kwa
kina akatupa taarifa kuhusu silaha hii,” alisema.
Alieleza, “Tulikwenda mpaka pangoni na kufanikiwa kupata SMG hii ikiwa
na magazini moja na risasi 20… silaha hii ni miongoni mwa zilizoporwa kwa
askari mwezi uliopita”.
Alisema licha ya kupatikana kwa silaha hiyo, watu kadhaa wanashikiliwa
wakihusishwa na tukio hilo.
Alisema upelelezi unaendelea kupata taarifa za kuwezesha kupatikana kwa
silaha nyingine na vitu mbalimbali vilivyowahi kuibwa.
“Naomba wakazi wa Tanga na Watanzania kwa ujumla muendelee kuvuta subira
na kutoa ushirikiano…endelezeni utulivu na mshikamano kwa jeshi la polisi ili
kwa pamoja tuweze kumaliza tatizo hili,” alisema.
Alisema upo umuhimu mkubwa kwa wananchi, kuendeleza utulivu kwa
kutokubali kuamini taarifa potofu zenye kujenga hofu, zinazosambazwa na baadhi
ya mitandao ya kijamii kwa kuwa zinalenga kuwavuruga.
“Kimsingi jeshi la polisi pamoja na vyombo vingine vya usalama,
linaamini na kuthamini kazi ya vyombo vya habari hasa vile makini, ambavyo
vimeendelea kuwaarifu wananchi habari sahihi ambazo hazina ghilba wala
kuwachanganya”, alisema.
Alikanusha taarifa zilizoenea mjini kwamba ipo miili ya wahalifu, iliyokutwa
ndani ya mapango hayo, kutokana na mapigano yaliyofanyika mwishoni mwa wiki.
“Ndugu zangu mwanzoni tulikuwa tukisikia harufu kali ya kama miili
iliyooza, kweli tulijitahidi kutafuta na tukafanikiwa kuona mizoga ya ngedere
na siyo binadamu ...wanyama hao walikuwa watatu na walikuwa na majeraha makubwa
sana. Kwa hiyo hawakuwa watu, bali ni ngedere ndio walikokuwa wamekufa na kuoza
humo pangoni,” alisema.
Akizungumzia mkakati wa kupata silaha iliyosalia na vifaa vingine
vilivyoporwa, Chagonja alisema jeshi lake na kikosi cha operesheni hakitalala usingizi
mpaka vitu vyote vipatikane.
No comments:
Post a Comment