Mtoto Yohana Bahati mwenye ulemavu wa ngozi
(albino), aliyetekwa katika Kijiji cha Ilelema wilayani Chato katika Mkoa wa
Geita, mwili wake umekutwa ukiwa
umefukiwa huku umenyofolewa miguu na mikono.
Polisi imesema baba mzazi wa mtoto huyo,
Bahati Misalaba na mkazi wa kitongoji cha Mapinduzi katika kijiji cha Lumasa,
wilayani Chato, wamekamatwa kwa ajili ya uchunguzi zaidi.
Mwili wa mtoto huyo mwenye umri wa mwaka na
miezi sita, ulikuwa umefukiwa katika moja ya mashamba ya mahindi ndani ya hifadhi, huku pembeni yake kukiwa na
kipande cha nguo kilichokuwa kimejaa damu.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Geita, Joseph
Konyo aliwaambia waandishi wa habari jana kwamba mwili ulipatikana juzi saa 12
jioni.
''Mwili wa mtoto huyu ulipatikana ukiwa
umefukiwa ndani ya kaburi dogo katika shamba la mahindi, mahali ambapo si
makazi rasmi ya kuishi watu wakati jeshi la polisi kwa kushirikiana na raia wema
walipokuwa katika harakati za kumtafuta baada ya kuwa ameibwa siku ya Jumapili
saa 2.00 usiku akiwa amebebwa na mama yake,'' alisema Kamanda Konyo.
''Eneo jirani na lilipokuwa kaburi la mwili wa
mtoto huyu kulikutwa kipande cha nguo chenye damu, lakini polisi walipofukua
walikuta miguu yote na mikono ikiwa imenyofolewa, hali iliyotulazimu kuamini
kuwa watekaji waliofanya ukatili huo watakuwa wameondoka na viungo hivyo,''
alisema.
Katika tukio hilo, watekaji waliokuwa na silaha mbalimbali za jadi, walimjeruhi
pia Ester Bahati (30), ambaye ni mama wa mtoto. Kwa sasa Ester amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya
Bugando.
''Msako tuliouendesha ulilenga kuokoa maisha
ya mtoto huyu, lakini hatukuweza kufanikiwa katika hilo badala yake tumempata
akiwa tayari amekwishafariki, hili ni tukio baya sana, lenye kuudhi lililojaa
ukatili usioweza kuvumilika kwa mtu yeyote anayeamini katika Mungu,” alisema
kamanda.
Aliahidi, “Tutaendelea kuwasaka wale wote
waliohusika katika tukio hili, wakiwemo waganga wa jadi, naamini tutawakamata
na siyo muda mrefu hakuna atakayebaki salama katika hili.''
Alitoa mwito kwa wananchi kutoruhusu tukio
lingine la namna hiyo litokee, badala yake wachukue hatua mapema kwa kutoa
taarifa kwa vyombo husika vya dola viweze kudhibitiwa.
Alisema kila mtu anapaswa kutambua wajibu kuwa
ulinzi na usalama ni suala la jamii nzima na siyo kuachia polisi peke yake.
Aidha alitaka waandishi wa habari kusaidia
kuibua matishio mbalimbali wanapokuwa wanatimiza majukumu yao hatua
zichukuliwe.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kijijini, familia
anayotoka mtoto huyo ina watoto wengine wawili wenye ulemavu wa ngozi ambao ni
Tabu Bahati (3) na Shida Bahati (12).
Wakati wa utekaji, watoto hao inaelezwa
hawakuwa nyumbani hapo, bali walikuwa wakicheza nyumba ya jirani. Baba yao
inadaiwa alikuwa nyumbani akiota moto.
Mama yao, Ester anaendelea kutibiwa majeraha yaliyotokana na
mapanga wakati akijaribu kumwokoa mtoto wake.
Hii ni mara ya pili ndani ya kipindi
kisichozidi miezi miwili, tangu tukio kama hilo lijitokeze baada ya mtoto Pendo
wa kijiji cha Ndami, Wilaya ya Kwimba, mkoani Mwanza, kutekwa na watu
wasiofahamika. Mtoto huyo hadi sasa hajapatikana.
Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa
nchini na Mkurugenzi Mkazi wa Shirika la Maendeleo la umoja huo
(UNDP), Alvaro Rodriguez amehimiza serikali kuchukua hatua zaidi, kukabili
mauaji ya watu wenye albinism.
Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari jana
kuhusu kuuawa kwa mtoto Yohana, Mratibu huyo wa UN alisema pamoja na juhudi
zilizopo sasa za kukabili mauaji dhidi ya watu wenye ulemavu huo wa ngozi, lazima ziongezwe.
Alisema katika kipindi cha miezi miwili,
Tanzania imeshuhudia kutekwa nyara kwa watoto wawili katika Kanda ya Ziwa,
akiwemo Pendo ambaye pamoja na juhudi za kumtafuta kuendelea, hadi sasa
hajajulikani aliko.
Alisema Umoja wa Mataifa unasikitishwa na
vitendo vya kikatili dhidi ya watoto hao wawili.
Mashambulio dhidi ya watu wenye albinism,
yanaelezwa kuwa yanasababishwa na imani za kishirikina na kwamba kutoka mwaka
2000 hadi sasa, watu 74 wenye ulemavu
huo wameuawa.
“Mashambulizi haya yanaambatana na ukatili
mkubwa, na wakati serikali inafanya kila juhudi kukabili tatizo hili,
juhudi kubwa zinastahili kufanywa ili
kukomesha mauaji na kulinda kundi hilo
dogo la watu ambao wako katika hatari kubwa," ilisema sehemu ya taarifa
hiyo.
Alisema mashambulio dhidi ya albino,
hayavumiliki, si halali kwa namna yoyote na yanaweza kukomeshwa.
Mratibu huyo alipongeza juhudi za serikali
katika kukabiliana na wimbi hilo la mauaji hayo.
Alisema Umoja wa Mataifa unataka mamlaka
husika, kuhakikisha haki za raia zinalindwa na utawala wa sheria unazingatiwa.
“Tunataka mwaka 2015 kuwa mwaka wa haki za
Watanzania wote zitaheshimiwa wakiwemo albino,” ilisisitiza.
Mratibu huyo wa UN alisema amezungumza na Mkuu
wa Mkoa wa Geita, Fatma Mwassa na Chama cha Maalbino ( TAS). Alisema alihakikishiwa kwamba
wanafanya kila linalowezekana, kukomesha madhila dhidi ya maalbino.
No comments:
Post a Comment