Askari wa Jeshi la Polisi amejeruhiwa na madereva wa
pikipiki maarufu kama bodaboda katika fujo zilizoibuka juzi jioni katika eneo
la Mzinga, Kongowe Mbagala nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam katika Manispaa
ya Temeke.
Akizungumza kwa njia ya simu kuhusiana na tukio hilo,
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Temeke, Kihenye Kihenya alisema askari walikuwa
kwenye doria kwa kutumia pikipiki maarufu kama Tigo na walipofika eneo la
Mzinga walimkamata dereva mmoja aliyebainika kuwa na matatizo kadhaa kwenye
pikipiki yake.
“Polisi walimkamata mwendesha pikipiki mmoja na
ikabainika kwamba alikuwa na makosa kadhaa ambayo yalimpasa alipe faini. Lakini
madereva wenzake walipoona amekamatwa wakaanzisha fujo na kumjeruhi mmoja wa
askari kwa kumpiga chupa usoni,” alisema Kihenya.
Aliongeza kuwa “Tumekamata bodaboda kumi na tano na
tayari tunaendelea na uchunguzi ili kuweza kubaini wahusika wakuu na tuweze
kuwafikisha mahakamani kwa kosa la shambulio,” alieleza.
Mashuhuda wa tukio hilo walisema fujo hizo zilikuwa
kubwa kiasi kwamba polisi walilazimika kuwatawanya washambuliaji kwa kupiga
risasi za moto hewani.
“Mimi nilifunga duka nikakimbia maana kulikuwa
hakukaliki hapa, walipompiga yule askari, uso wote ulitapakaa damu ndipo
wakarusha risasi hewani. Kila mtu alikimbilia anakojua mwenyewe,” alisema moja
wa mashuhuda aliyeogopa kutajwa jina lake.
Kwa upande wake, Sanja Justin, alisema yeye alikuwa
ana safari ya kwenda Mbagala na alipokaribia kituoni cha basi, alisikia mlio wa
risasi na kuamua kukimbia na kurudi nyumbani. “Nilitaka kwenda kupanda gari
nielekee Mbagala lakini nilipofika karibu na kituo nikasikia mlio wa risasi,
nikarudi mbio na kila mtu alikuwa kwenye harakati za kukimbia ili kujiokoa na
matatizo,” alisema.
Eneo la Mziga limekuwa na matukio mengi ya kihalifu
ambapo mwishoni mwa mwaka jana kuliibuka kikundi cha kihalifu kilichojiita
Black Amerika na kusababisha ukosefu wa usalama katika eneo hilo. Hata hivyo
Jeshi la Polisi lilifanikiwa kulidhibiti kundi hilo na kurejesha hali ya
utulivu kwa wakazi wa eneo hilo.
(Picha ya Maktaba).
No comments:
Post a Comment