Viongozi wa madhehebu ya dini jijini Mwanza,
wakiwamo Maaskofu na Mashehe jana walijikuta wakibubujikwa na machozi baada ya
kumtembelea Ester John, ambaye amelazwa Hospitali ya Rufaa ya Bugando.
Ester amelazwa
baada ya kujeruhiwa vibaya na watu wasiofahamika, ambao walimteka
mwanawe mwenye ulemavu wa ngozi
(albino), Yohana Bahati na kutokomea naye kusikojulikana.
Viongozi hao
wakiwemo maaskofu 10 na mashehe 10 walimtembelea Ester hospitalini hapo,
ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kongamano kubwa la amani linalotarajiwa
kufanyika Februari 28 mwaka huu kuiombea nchi amani na kulaani mauaji ya
albino.
Mashehe na maaskofu hao walimuombea dua na
sala Ester aweze kupona haraka na
walilaani kitendo cha kinyama, alichofanyiwa na wauaji hao.
Waliiomba Serikali ichukue hatua za haraka
kukomesha mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi nchini.
Akizungumza hospitalini hapo huku akitokwa na
machozi katika Wadi Namba 9 alikolazwa Ester, Mwenyekiti Mwenza wa Kamati ya
Amani ya Mkoa ya Viongozi wa Dini, Shehe Hassan Kabeke alisema wanaungana
kwa pamoja kulaani matukio mawili ya kinyama ya kuuawa kwa mtoto Yohana na
kujeruhiwa vibaya mama yake mzazi.
“Maneno ya kusema yananiishia baada ya kumuona
Ester, mimi nadhani hakuna sababu ya kuremba maneno dhidi ya ukatili huu wa
kinyama, nasikia maumivu makali sana ndani ya moyo wangu kama kiongozi wa
kiroho, tunaitaka serikali katika hili isiondoe adhafu ya kifo kwa kisingizio
cha haki za binadamu”, alisema.
Aliongeza “Tunapozungumzia haki za binadamu,
maana yake ni usawa, ukweli na haki kwa watu wote nchini, haiwezekani watu
wengine waue watu halafu tunasingizia haki za binadamu, na wao wahukumiwe
adhabu ya kifo, katika hili msimamo wetu kama viongozi wa dini tunaomba adhabu
ya kifo isiondolewe”.
Pia, aliwataka majaji wanaosikiliza kesi za
watu wenye ulemavu wa ngozi, kuzisikiliza kwa wakati ili kuondoa ucheleweshaji
wa kesi hizo ili hukumu zitolewe kwa wakati.
“Nichukue fursa hii kwa niaba ya wenzangu
kuwaomba waheshimiwa majaji waharakishe kusikiliza mashauri yaliyoko mahakamani
yanayohusisha mauaji ya watu wenye ulemavu wa ngozi (albino)”, alisema.
Kwa upande wake, Katibu Mwenza wa Kamati hiyo
ya Amani, Askofu Zenobius Isaya alimtaka Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini
(IGP), Ernest Mangu kulichukulia suala
la mauaji ya albino kwa uzito wa kipekee kwa vile linagharimu maisha ya watu
wasio na hatia katika jamii.
“Tunamuomba IGP Mangu alichukulie suala hili
kwa uzito mkubwa, afanye uchunguzi wa kina ili aweze kukomesha mauaji haya ambayo
yameipaka matope nchi yetu mbele ya Jumuiya ya Kimataifa”, alisema.
Akitoa salaam kwa Ester ambaye aliweza kukaa
kitandani kwa muda, Isaya alisema shida iliyomkuta ni shida ya Watanzania wote
wenye kupenda amani na kuchukia maovu.
“Shida iliyokukuta na taabu yako ni taabu yetu
sisi sote wapenda amani ; na sisi wapenda amani kwa wingi wetu, kama
unavyotuona, tunalaani tukio hili la kinyama, jambo hili ni la kinyama lakini
tunakutia moyo uweze kupona haraka na Mungu akupe moyo wa uvumilivu katika
kipindi hiki kigumu,” alisema.
Aliushukuru uongozi wa Hospitali ya Bugando
kwa kufanya kazi kwa uvumilivu na kutanguliza upendo katika kumhudumia Ester
tangu alipolazwa hospitalini hapo Februari 17 mwaka huu.
“Nichukue fursa hii kuwashukuru sana madaktari
na wauguzi wetu kwa kuwa bega kwa bega na Ester kwa kumhudumia bila ya kuchoka,
hii inaonyesha kuwa na mshikamano na Mungu awabariki”, alisema.
Awali, akiupokea ujumbe huo, Mkurugenzi wa
Utawala na Fedha wa Hospitali ya Bugando, Leah Kagina aliwashukuru viongozi hao
wa dini kwa kuamua kutenga sehemu ya muda wao kwa kwenda kumjulia hali.
Alisema hiyo ni mara ya kwanza kwa hospitali
hiyo kupokea ujumbe huo mkubwa kwenda kumjulia hali Ester.
“ Tunawashukuru sana kwa ujio wenu, ni kwa mara ya kwanza kwa hospitali kupokea
ujumbe huu mzito wa viongozi wa kiroho kwa ajili ya kuja kumjulia hali Ester,
hii inadhihirisha ni jinsi gani mlivyo na upendo kwa watu wote, rai yangu kwenu
niwaombe mtumie ibada zenu katika kutoa elimu kwa jamii dhidi ya mauaji haya”,
alisema.
Alisema kuwa viongozi wana nafasi kubwa katika
kuelimisha jamii juu ya imani potofu, ambazo zimekuwa zikienezwa dhidi ya
mauaji hayo na kuitaka serikali kuwachukulia hatua stahiki wauaji wa watu wenye
ulemavu wa ngozi.
Akizungumzia hali ya mgonjwa, Muuguzi wa Zamu
katika wadi Namba 9, alikolazwa Esta, Adolphina Kishumba alisema hali ya Ester
kwa sasa inaendelea vizuri na anajitahidi kula chakula.
“Kwa hivi sasa hali ya Ester inaendelea
vizuri, ni tofauti na alivyokuwa mwanzo na sasa hivi anakula na anaanza
kutembea kwenda chooni”, alisema.
Mama mzazi wa Ester ambaye anamuuguza
hospitalini hapo, Tabu Mang’enyi aliwashukuru Watanzania kwa misaada yao ya
hali na mali wakati wote, ambao amekuwa na mwanawe hospitalini hapo.
“Nawashukuru Watanzania wote kwa kumuombea
mwanangu na kuendelea kumjulia hali. Kutokana na maombi yenu hali ya mwanangu
inaendelea vizuri”, alisema.
No comments:
Post a Comment