AJIRA 40,735 ZAZALISHWA MIEZI MITATU


Ajira 40,735 zimezalishwa ndani ya miezi mitatu kuanzia Oktoba hadi Desemba mwaka jana na kufanya jumla ya ajira 173,787 kupatikana kwa kipindi cha nusu mwaka kuanzia Julai hadi Desemba mwaka jana.

Wizara ya Kazi na Ajira imesema ongezeko hilo la ajira limejitokeza katika maeneo makuu mawili ikiwemo ajira serikalini ambazo ni 2,652 sawa na asilimia 6.5 na ajira kupitia sekta rasmi binafsi ambazo ni 38,083 sawa na asilimia 93.5.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Msemaji wa Wizara hiyo, Ridhiwan Wema alisema takwimu hizo zinaonesha kwamba sekta binafsi imeendelea kuwa mhimili wa uzalishaji wa ajira nchini kutokana na serikali kuendelea kuweka mazingira wezeshi ya waajiri kuongeza fursa za ajira kwa Watanzania.
“Katika kipindi cha nusu mwaka  sekta binafsi rasmi ambayo ndiyo mwajiri mkuu ilizalisha ajira 173,787 kupitia uwekezaji binafsi ambapo uwekezaji kupitia ujenzi zilizalishwa ajira 107,527, uwekezaji kupitia  Kituo cha Uwekezaji (TIC) ajira 34,184 na Sekta ya Mawasiliano ajira 342” alisema.
Alisema hatua zinazochukuliwa kwa sasa ni pamoja na kufanya marekebisho ya Sera ya Ajira ya 2008, Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Namba 6,2004, Sheria ya Taasisi za Kazi namba 7,2004 pamoja na kutunga sheria Mpya ya Ajira za Wageni ambayo imelenga kulinda ajira za Watanzania, kuboresha mazingira ya biashara na kuhamasisha uwekezaji.
Alishukuru wadau mbalimbali kwa ushirikiano wao kwa kutoa taarifa za ajira kwa wakati. Alitoa mwito kwa waajiri wote nchini kutoa ushirikiano katika ukusanyaji taarifa za soko la ajira.
“Taarifa hizi zimelenga kuiwezesha serikali kujua hali ya ajira nchini na kuchukua hatua stahiki ikiwa ni pamoja na kuwezesha serikali kupanga matumizi sahihi ya nguvu kazi nchini,” alisema.
Alisema taarifa hizo ni miongoni mwa vigezo vikuu vinavyotoa picha halisi ya mafanikio ya kiuchumi na kimaendeleo kwa nchi au mahali husika na zinasaidia kupanga, kutekeleza na kupima ufanisi wa mipango ya kiuchumi nchini pamoja na kupima uwezo wa kiuchumi katika wakati husika.

No comments: