AFUNGWA MAISHA JELA KWA KUNAJISI MTOTO WA MIAKA MINNE


Mkazi wa kijiji cha Makutupa kata ya Lupeta wilaya ya Mpwapwa mkoani Dodoma, Yusuph Chatambala (45) amehukumiwa kifungo cha maisha gerezani baada ya kukiri kumnajisi mtoto mwenye umri wa miaka minne.

Ilidaiwa mahakamani kwamba mwanamume huyo alimpatia mtoto huyo wa kike Sh 500  asitoe siri baada ya kumnajisi, Februari 20, mwaka huu.
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, mwanamume huyo alitenda kosa hilo baada ya kumkamata mtoto huyo akicheza na watoto wenzake jirani na nyumbani kwao, kisha kumpeleka kwenye shamba la mahindi na kumnajisi.
Hukumu dhidi ya mshitakiwa huyo,  ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpwapwa,  Pascal Mayumba baada ya kumtia hatiani mshtakiwa kutokana na kukiri mashitaka.
Akisoma hukumu, Hakimu alisema siku ya tukio, Chatambala baada ya kumaliza alimpatia mtoto huyo Sh 500 na kuondoka zake huku akiwa amemjeruhi mtoto huyo sehemu za siri .
Alisema  kutokana na mshtakiwa kukiri kosa, kwa mujibu wa sheria,   mtu yeyote anayefanya kosa la kumbaka mtoto chini ya miaka 10 anastahili kifungo cha maisha jela.
Alipopewa nafasi ya kujitetea kabla ya hukumu, mshtakiwa alikiri kufanya kitendo hicho. “Kweli mheshimiwa mimi nakiri kutenda kosa hilo hivyo naomba Mahakama yako inisamehe tu sitarudia tena,” alidai.
Mwendesha Mashitaka  wa Polisi,   Godwin Ikema  aliomba Mahakama itoe adhabu kali  iwe fundisho kwa watu wenye tabia kama hiyo.
Hakimu Mayumba alisema   kutokana na  kosa kuwa la  kikatili   na kwa kuzingatia sheria,  Mahakama inampa adhabu ya  kutumikia  kifungo  cha maisha gerezani.
Alisema kwa mtu yeyote ambaye hajaridhika na adhabu hiyo, ana haki ya kukata  rufaa ndani ya siku 30. Hakimu alipokuwa akitoa hukumu hiyo  mahakamani, mshitakiwa huyo alikuwa akitokwa machozi.
Kwa mujibu wa hati ya mashitaka, alimfanyia kitendo hicho Februari 20 mwaka huu saa 12:00 jioni katika kijiji cha Makutupa.

No comments: