Mamlaka
ya Mapato Tanzania (TRA) kupitia Idara ya Forodha, imekamata mali ya magendo
iliyokuwa ikiingizwa nchini kinyemela kupitia bandari bubu ya Kunduchi, jijini
Dar es Salaam.
Naibu
Kamishna wa Forodha, Patrick Kisaka ametaja mali hizo kuwa ni mifuko 40 ya
sukari kutoka Brazil, ndoo 20 za mafuta ya kupikia kutoka Mashariki ya Mbali na
katoni 70 za vigae, ambavyo maofisa wa TRA kwa kushirikiana na askari wa doria,
walivikamata Januari 8 katika bandari
hiyo.
Akizungumza
na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kamishna huyo aliwataka
wananchi hususan wanaoishi maeneo ya mipaka na ukanda wa Pwani ya Bahari ya
Hindi, kutojihusisha na biashara ya magendo na badala yake kuwafichua watu
wanaofanya biashara hizo ambao wanaikosesha Serikali mapato.
“Tunaomba
watu wanaojihusisha na biashara hizi waache mara moja kabla hawajaangukia
mikononi mwetu kwani tutawachukulia hatua za kisheria zikiambatana na kifungo
au faini, na huu ni kwa mujibu wa sheria.” Alisema Kamishna huyo.
Aidha,
Kamishna huyo aliwataka wananchi watoe taarifa kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania
(TRA) kupitia namba 0789 933 8930 na 0789 338 931 endapo watabaini kuna vitendo
vyovyote vya kimagendo hasa kwenye maeneo ya mipaka, ambako biashara hiyo
imekuwa ikifanyika kwa kasi na kuahidi zawadi nono itakayolingana na kiwango
cha kodi ya bidhaa hiyo.
Kisaka
aliwahakikishia wananchi kuwa idara yake
kwa kushirikiana na askari wa doria wataendelea kupambana na wafanyabiashara wa
magendo katika maeneo ya majini na nchi kavu usiku na mchana ili kuhakikisha
Serikali inapata mapato yake, ambayo yamekuwa yakipotea kwa njia hizo za
kimagendo.
‘Sisi
tutaendelea kupambana na magendo kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi kwa
kutumia rasilimali zetu za nchi kavu na majini. Wenzetu wana boti sisi tutaweka
mafuta na kufanya doria katika mipaka yote ya majini na nchi kavu”, alisisitiza
Kamishna huyo.
Katika
kipindi kisichozidi mwaka mmoja, TRA kupitia idara hiyo imeshakamata mifuko
1158 ya sukari ya kilo 50 kutoka nje ya nchi, iliyokuwa ikiingizwa kwa magendo
nchini kupitia doria zake mbalimbali zilizoko maeneo ya mipakani na kuahidi
kuendeleza mapambano hayo.
Bandari
bubu zinazotajwa kuwa ni kinara wa kupitisha bidhaa kimagendo ni Kunduchi na
Ununio jijini Dar es Salaam na Mlingotini ya Bagamoyo.
No comments:
Post a Comment