Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Magesa Mulongo ametoa
siku tano kuanzia juzi Jumatatu kwa watendaji, sungusungu na wakazi wa kijiji
cha Ndami, tarafa ya Mwambashimba wilayani Kwimba kuhakikisha mtoto mwenye
ulemavu wa ngozi, Pendo Emmanuel (4) aliyeporwa na watu wasiojulikana
anapatikana akiwa hai ama mwili wake.
Alitoa agizo hilo wakati akizungumza na wakazi wa kijiji hicho
na watendaji wa wilaya ya Kwimba ambapo alisema mazingira hayaoneshi kama
mlango ulipigwa jiwe kubwa maarufu kama ‘fatuma’.
Alisema Kwimba ina watu 74 wenye ulemavu wa
ngozi huku mtoto Pendo jina lake likiwa la tisa, lakini inashangaza kusikia
siku ya tukio, Desemba 27 mwaka jana majira ya saa 3 usiku sungusungu wote
walikwenda kula na muda mfupi baadaye mtoto huyo aliibwa baada ya kuvamia
nyumba aliyokuwamo.
Alihoji maelezo ya sungusungu hao kwamba siku
hiyo, wakati wa mchana walionekana watu wanne wasiofahamika wakiwa na pikipiki,
lakini hakuna aliyechukua tahadhari ilhali wakijua kijijini hapo kuna mtu
mwenye ulemavu wa ngozi.
“Hii hainiingia akilini, mimi nasema hapana
kwa sungusungu na wanakijiji wote, lipo jambo halijafanyika na kwa imani yangu
Pendo yupo salama na apatikane ndani ya siku tano, Ijumaa nitarudi hapa,”
alisema Mkuu huyo wa Mkoa.
Mulongo alitaka kila mmoja ajiulize katika
nafsi yake, Pendo yupo na kwanini watu wengine wapo salama na bado watendaji
wote wanaongea lugha inayofanana.
“Jambo la hovyo ni mazingira tuliyosoma kwenye
eneo la tukio kuwa wahusika walikwenda na ‘fatuma’, lakini hakuna mazingira
yoyote yanayoonesha kuwa fatuma lilitumika, hakuna nguvu iliyotumika bali yapo
mazingira mnayafahamu, hata viongozi wa eneo hilo wanataka kutuaminisha hivyo,”
alisema na kuongeza:
“Leo tarehe 5 (juzi), nasema hakuna kulala
natoa siku tano kuanzia leo hadi Ijumaa Pendo apatikane, sungusungu maneno
yasiwe mlikwenda kula chakula, mnatokaje kwenye lindo wote kwa pamoja, nataka
kumuona Pendo akiwa mzima, najua.
Aliongeza: “Hamuwezi kujitangaza wenyewe kuwa
ni watu wakatili, mazingira yanaonesha tukio limetengenezwa na hatuwezi kuwa na
kijiji kisichoona uchungu kwa binadamu mwenzao, mhusika mnamjua na mnamficha”.
Alisema dunia nzima inawatazama watu wa Kwimba
na Mwanza kwa ujumla kama watu wa hovyo wasio na utu hata kidogo kutokana na
uzembe wa watu wachache, huku akisisitiza hatakubali mambo hayo yaendelee
kutokea.
Alisema jambo hilo halihitaji itikadi ya vyama
vya siasa, bali kuona maisha ya Pendo yanaokolewa.
Naye Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza,
Valentino Mlowola alisema haiwezekani mtu kutoka mbali kufika katika eneo hilo
na kumchukua mtoto Pendo bila kuongozwa na mwenyeji, hivyo kuwataka wananchi
kutoa ushirikiano.
Alisema Serikali ina mkono mrefu hivyo
waliofanya kitendo hicho lazima watapatikane na kwamba Jeshi la Polisi
halitolala hadi mtoto huyo apatikane akiwa hai au mwili wake.
Mtoto Pendo aliporwa na watu wasiojulikana
usiku wa Desemba 27 majira ya saa 4.30 usiku katika kijiji Ndama wilayani
Misungwi baada ya watu hao kuvunja mlango kwa kutumia jiwe kubwa maarufu kama
‘fatuma’.
Watu 15 akiwamo baba mzazi wa mtoto huyo
wanashikiliwa na polisi mkoani hapa kwa uchunguzi zaidi.
No comments:
Post a Comment