Sasa ni rasmi kwamba, majaribio ya usafirishaji wa gesi asilia
kutoka Mnazi-Bay mkoani Mtwara kwenda Dar es Salaam, yanatarajiwa kuanza mwezi
ujao.
Hiyo inatokana na
kukamilika kwa kiasi kikubwa kwa mradi wa ujenzi wa miundombinu ya gesi asilia.
Kutokana na hatua
hiyo, Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC),
limeelezea kuridhishwa hatua hiyo, huku Mwenyekiti wake, Michael Mwanda akisema
sasa ataanza kupata usingizi.
Kuthibitika
kuanza kwa majaribio hayo mwezi ujao kumeelezwa na Kaimu Meneja Mkuu wa kampuni
tanzu ya TPDC, Kampuni ya Gesi ya Taifa (GASCO), Kapuulya Musomba wakati wa
ziara ya wajumbe wa Bodi ya TPDC waliokagua maendeleo ya ujenzi huo mwishoni
mwa wiki katika mikoa ya Dar es Salaam, Lindi na Mtwara.
Walikagua vya
kupokelea gesi Kinyerezi na Tegeta, Dar es Salaam, vituo vya udhibiti wa
usalama wa miundombinu ya bomba vilivyojengwa kuanzia Mtwara hadi Dar es Salaam
kwa umbali wa kilometa 30, kituo cha kupokea gesi cha Somanga Fungu wilayani
Kilwa, MnaziBay mkoani Mtwara inakopatikana gesi na pia kijiji cha Madimba,
Mtwara unakojengwa mtambo wa kuchakata gesi.
Akizungumzia
maendeleo ya mradi huko, Musomba alisema unakwenda vizuri na kwamba kwa hatua
iliyofikiwa, sasa majaribio yanaweza kuanza mwezi ujao.
“Pamoja na
changamoto kadhaa, naweza kusema tumefika pazuri na wakati wowote mwezi ujao
majaribio ya kusafirisha gesi yanaweza kuanza…nia yetu ni kuhakikisha kama
ilivyokuwa imepangwa, Juni mwaka huu tuwe tumekabidhi mradi kwa serikali,”
alisema Musomba.
Kutokana na kauli
hiyo ya msimamizi mkuu wa mradi, Mwanda alisema kutokana na kazi hiyo mradi huo
utakamilika kama ulivyopangwa Juni, mwaka huu. Maelezo hayo yalimkuna Mwanda na
kusema: “Tujaribu kuwaeleza wananchi juu ya maendeleo ya mradi, kwamba
unakwenda vizuri. Binafsi nitaanza kupata usingizi maana shughuli ilikuwa ngumu
na upinzani ulikuwa mkubwa. Sasa kazi inakamilika, tujitahidi kuwa wazalendo…”
Awali, Musomba
alisema ujenzi wa bomba hilo lenye urefu wa kilometa 506 umekamilika kwa
asilimia 99 na wameshajaribu kwa kupitisha maji.
"Kwa upande wa ujenzi wa
bomba umekamilika kwa asilimia kubwa, na wameshapitisha maji kuangalia kama
kuna maeneo yanayovuja, kinachofanyika sasa ni kukausha maji hayo kazi ambayo
itakamilika mwisho wa mwezi huu," alisema na kuongeza kuwa, miundombinu
mingine kama majengo katika maeneo ya miradi na mitambo viko katika hatua za
mwisho. Mradi huo unagharimu dola za Marekani bilioni 1.225, sawa na Sh
trilioni 2.08 za Kitanzania .
No comments:
Post a Comment