Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba,
amebainisha sera zake pindi Watanzania watakapompatia nafasi ya kuiongoza
Tanzania na kusisitiza kupambana na rushwa, urasimu, udini na ajira.
Aidha, Waziri
huyo ambaye hivi karibuni alitangaza rasmi nia yake ya kuwania nafasi ya Urais
kupitia chama chake cha CCM, katika uchaguzi mkuu unaotarajiwa kufanyika mwaka
huu, alitaja maeneo mengine atakayoyapa kipaumbele katika uongozi wake huo.
Baadhi ya maeneo
hayo ni pamoja na nishati miundombinu, mikopo, kanda ya kiuchumi, afya, huduma
za maji, elimu, matatizo ya walimu na maisha ya Watanzania kwa ujumla.
Katika mahojiano
aliyoyafanya na Padri Privatus Karugendo aliyeandika kitabu cha Mazungumzo ya
January Makamba, alisema katika eneo la urasimu endapo atapatiwa fursa ya
kuiongoza nchi hiyo atahakikisha anafumua upya mfumo wa utumishi na utendaji
serikalini ili kukomesha urasimu uliokithiri serikalini.
“Katika kufanya
hili, ni lazima tuongozwe na misingi ifuatayo: Kwanza, uwajibikaji. Kwa sasa,
ni vigumu sana kuwawajibisha watumishi wa umma kwa uzembe, ubadhirifu au
kutotimiza wajibu wao. Tubadilishe Sheria ya Utumishi wa Umma ili kupunguza
mlolongo wa kufikia maamuzi ya kuwawajibisha watu,” alisema January.
Katika eneo la
rushwa, alisema kutokana na hali ya sasa ya rushwa kukithiri nchini, endapo
atapatiwa nafasi anatarajia kufumua na kujenga upya Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa (Takukuru), mifumo na sheria za kudhibiti na kuadhibu vitendo
vya rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma.
Alisema katika
mabadiliko hayo makosa ya rushwa na ubadhirifu wa mali ya umma yatakuwa ni
makosa ya uhujumu uchumi na uhujumu wa taifa, na adhabu yake itaongezeka.
Kuhusu ajira
January alisema eneo hilo linahitaji msukumo na hatua za kimapinduzi, na sio
maneno tu ya kurudia kauli kwamba ajira kwa vijana ni bomu, lakini bila kutoa ufumbuzi.
Alipendekeza
hatua za kumaliza tatizo hilo kuwa ni Bunge lipitishe Muswada Maalum, Muswada
wa Matumizi kwa Uwezeshaji Kiuchumi kwa Vijana, ambao utakuwa ni sheria maalumu
ya matumizi ya Sh trilioni 3.6 kwa ajili ya mkakati wa miaka mitatu wa kupanua
ajira kwa kuchochea shughuli za uzalishaji mali na uchumi.
“Katika eneo la
elimu, kwanza nitahakikisha mjadala uliopo kuhusu dira ya elimu, ni elimu gani,
ya aina gani na katika lugha ipi – tunataka watoto wetu wapate? Ni nini maana
na malengo ya elimu nchini mwetu? Tukimaliza mjadala huu na sote tukakubaliana
kama taifa, tutaondokana na changamoto ya kubadilisha mtaala mara kwa mara kama
ilivyo desturi sasa,” alisema.
Aidha alisema iko haja ya
kuanzisha Wizara mahususi ya Maendeleo ya Jiji la Dar es Salaam ili kuwezesha
miradi mikubwa ya uwekezaji katika jiji kutekelezwa kwa haraka.
No comments:
Post a Comment