Bei ya mafuta ya petroli,
dizeli na mafuta ya taa, imeshuka kuanzia kesho, huku watumiaji wa petroli
wakipata nafuu zaidi kutokana na kuuzwa chini ya Sh 2,000 baada ya kipindi cha
muda mrefu.
Kutokana na kushuka kwa bei
ambako pia kunachangiwa na kushuka kwa bei katika soko la dunia, sasa petroli
itauzwa lita moja kwa Sh 1,955, dizeli itakuwa Sh 1,846 kwa kila lita moja na
mafuta ya taa yatakuwa yanauzwa kwa Sh 1,833 kwa kila lita moja.
Hayo yalisemwa jana na
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura),
Felix Ngamlagosi alipokuwa akizungumzia mwenendo wa bei za mafuta nchini pamoja
na utangazaji wa bei mpya za mafuta.
Alisema kuanzia kesho
kutakuwa na punguzo la Sh 74 kwa petroli, Sh 62 kwa dizeli na Sh 54 kwa mafuta
ya taa.
“Kwa bei ya kesho (leo)
katika soko la Dar es Salaam hakutakuwa na mafuta ya zaidi ya Sh 2000. Kutakuwa
na punguzo la Sh 74 kwa petroli, Sh 62 kwa dizeli na Sh 54 kwa mafuta ya taa,”
alisema.
Alisema gharama za mafuta
yatakayokwenda mikoani zitaongezeka kutokana na usafiri.
Alisisitiza kuwa, Ewura
itahakikisha kuwa gharama zilizotangazwa ndizo zitakazotumika kwa wananchi.
Mkurugenzi huyo alisema bei
ya mafuta ya mwezi Januari nchini, ni bei katika soko la dunia iliyotumika
mwezi mmoja uliopita.
“Kwa Tanzania bei ya Desemba
ni ya mafuta ya Oktoba hapa nchini na bei za Novemba ndizo zitatumika kesho
(leo) hapa nchini,” alisema.
Alisema katika kipindi cha
robo ya mwisho wa mwaka kuanzia Septemba hadi Desemba mwaka jana, bei za mafuta
ghafi zimekuwa zikishuka kwa kasi ikilinganishwa na kipindi cha nyuma, bei
zimeshuka kutoka dola 100 (Sh 170,000) kwa pipa hadi kufikia wastani wa dola 60
(Sh 102,000) kwa pipa moja ambayo ni sawa na kushuka kwa bei kwa asilimia 40.
Kwa maelezo yake, asilimia
ya kushuka kwa bei katika soko la ndani ni tofauti na kushuka katika soko la
dunia kwa sababu mchango wa bei za soko la dunia katika bei za soko la ndani ni
takribani asilimia 60.
“Gharama nyingine kodi za
serikali, gharama za usafirishaji, gharama za usambazaji na gharama za upokeaji
mafuta ambazo huchangia katika bei hazikushuka kwa sababu hazitegemei kushuka
kwa bei za soko la dunia,” alisema.
No comments:
Post a Comment