BENKI YA MKOMBOZI YATINGA KWA KISHINDO SOKO LA HISA DAR


Hisa za benki ya biashara ya Mkombozi,  jana ziliingia kwenye  Soko la  Hisa la Dar es Salaam  (DSE) kwa kishindo huku bei yake ikipanda kwa asilimia 50 kutoka Sh 1,000 hadi 1,500.

"Haya ni mafanikio makubwa kwa benki yetu...kama nilivyosema mwanzoni wanahisa na watanzania kwa ujumla wana imani na matarajio makubwa kwenye hii benki," alisema Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mkombozi,  Masha Mshomba.
Mshomba alisema benki ya Mkombozi japokuwa ina muda mfupi tangu kuanzishwa kwake, imeonesha mafanikio makubwa na huku ikikua kwa kasi kubwa.
Alisema benki hiyo ilitegemea kupata Sh bilioni 5 kutokana na mauzo ya hisa 5,000,000, lakini ilifanikiwa kuuza hisa 3,780,000 na kupata Sh bilioni 3.78 kwa kipindi cha wiki tatu za mauzo ya hisa.
 Mkurugenzi  Mtendaji  wa DSE, Moremi Marwa, akiikaribisha Benki ya Mkombozi sokoni, alisema soko limejipatia mafanikio makubwa mwaka huu kuliko wakati wowote tangu kuanzishwa kwake miaka 16 iliyopita.
Benki ya Mkombozi inakuwa kampuni ya 21 kuuza hisa katika soko la Dar es Saalam na kuupandisha mtaji wa jumla wa soko kwa makampuni yote na kufikia Sh trilioni 21.
Akizungumza katika hafla hiyo,  Mkurugenzi  Mtendaji wa Swissport, Gaudence Temu alisifia uamuzi sahihi wa benki ya Mkombozi kuingia kwenye soko la hisa, ambapo alisema kuna faida nyingi za kibiashara.
"Tofauti na urahisi wa kupata mtaji kwa ajili ya biashara, kwenye soko la hisa kuna unafuu wa kodi lakini pia kuna umaarufu. Siyo kila kampuni inaweza kuuza hisa kwenye soko hili na hivyo basi uwepo wenu humu ni kielelezo kuwa benki yenu inakidhi vigezo," alisema  Temu.

No comments: