Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar imesema taasisi mbalimbali za kimataifa
zinazojishughulisha na masuala ya mafuta na gesi zimeanza kujitokeza kuomba
fursa ya kuwekeza katika sekta hiyo.
Maombi hayo
yamekuja kutokana na suala la mafuta na gesi kuondolewa katika orodha ya mambo
ya Muungano katika mchakato uliomalizika hivi karibuni wa Katiba
Inayopendekezwa na Bunge Maalumu la Katiba.
Hayo
yalisemwa na Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi wakati alipozungumza
na wananchi wa jimbo la Kitope huko Kichungwani mkoa wa Kaskazini Unguja, baada
ya kushiriki kazi za usambazaji majisafi na salama.
Balozi Iddi
ambaye ni mbunge wa jimbo hilo alisema miongoni mwa mambo ambayo yalikuwa
yakipigiwa kelele na wananchi wengi wa Zanzibar kuondolewa katika orodha ya
Muungano ni suala la mafuta na gesi.
“Wananchi
mambo ambayo tumeyapigania kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba yanaondolewa
katika orodha ya mambo ya Muungano ni suala la mafuta na gesi,” alisema.
Alisema
hatua hiyo imeanza kuleta manufaa makubwa kutokana na baadhi ya wawekezaji,
taasisi na mashirika ya kimataifa yanayojishughulisha na kazi za utafutaji wa
nishati hiyo kuwasilisha maombi yao.
Aidha,
balozi aliwataka wananchi kutokubali kuyumbishwa na kudanganywa na wanasiasa
ambao hivi sasa wamekuwa wakifanya kazi kubwa kuwababaisha wananchi na kupita
kila sehemu wakidai kwamba katiba inayopendekezwa haina maslahi kwa wananchi wa
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment