WALIOKUFA LORI LA PETROLI WAFIKIA WATANO, POLISI ALIYEJARIBU KUZUIA AAMBULIA KIPIGO



Idadi ya watu waliokufa kutokana na ajali ya moto wa lori lililopinduka na kisha kulipuka baada ya watu kulivamia kwa lengo la kujipatia mafuta, imeongezeka na kufikia watano kutoka vitatu vya awali.
Hayo yamethibitishwa na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova.
Alisema katika ajali hiyo iliyotokea juzi usiku eneo la Mbagala, watu 16 walijeruhiwa baada ya kuungua maeneo mbalimbali ya miili yao.
Ajali hiyo ilihusisha lori aina ya Scania lenye namba za usajili T 347 BXG mali ya Moil Transporter lililokuwa likitarajiwa kusafirisha mafuta kuelekea Kampala, Uganda likiwa na kemikali aina ya petroli lita 38,000 inayokadiriwa kuwa na thamani ya dola 36,000 (Sh milioni 60).
Aliwataja waliokufa kuwa ni Hassan Mohammed (25), mkazi wa Mbagala Kimbangulile, Masoud Masoud (33), Mohammed Ismail (19), Ramadhani Khalfan (36) na Maulid Rajabu, wakazi wa Mbagala Charambe.
Majeruhi waliotambuliwa ni Hamis Ally (35), mkazi wa Mbagala Kiburugwa, Rajabu Selemani (28), mkazi wa Tandika, Idd Said (28), Janney Mathayo (25), mkazi wa Mbagala Kizuiani, Mathayo Daniel (21), mkazi wa Mbagala Charambe na askari polisi, Koplo Thomas aliyejeruhiwa na jiwe kwenye paji la uso wakati akijaribu kuzuia vibaka kuchota mafuta kabla ya kulipuka.
Alisema majeruhi wengine 10 wamelazwa katika hospitali ya Taifa Muhimbili na Hospitali ya Wilaya ya Temeke wakiendelea na matibabu na wengi wao hali zao siyo za kuridhisha.
Kamanda Kova aliongeza kuwa, mbali ya kusababisha vifo na majeruhi, ajali hiyo pia ilisababisha kuungua kwa nyumba ya kulala wageni iitwayo United yenye vyumba 32, mali ya Deus Kasigwa (42), mkazi wa Mtoni Mtongani. Moto huo uliteketeza pia maduka matano yenye vitu vyenye thamani ya Sh milioni 197 na pipikipiki saba ziliteketea kabisa na moto.
Naye Ofisa Uhusiano wa Hospitali ya taifa ya Muhimbili, Doris Ishenda alisema majeruhi 11 wanaoendelea kutibiwa hospitalini hapo, huku akiongeza kuwa, hali zao sio nzuri kwa kuwa waliunguzwa vibaya na moto na kwamba madaktari wanaendelea kuwapatia matibabu.
‘’Majeruhi wote wamelazwa katika wadi namba 22 ya Sewa Haji wanaendelea na matibabu, lakini hali zao sio nzuri kabisa kwani waliungua sana,’’ alisema Ishenda.
Wakati huo huo, Paulo Milanzi (35), mkazi wa Chanika katika manispaa ya Ilala anayetuhumiwa kushiriki katika mauaji ya Ofisa Usalama wa Taifa, Sylvanus Mzeru, amefariki dunia baada ya kupigwa risasi katika majibizano na polisi.
Kova alisema mtuhumiwa huyo alikuwa akitafutwa na polisi kwa muda mrefu kuhusu matukio mbalimbali ya mauaji na unyang’anyi wa kutumia silaha jijini Dar es Salaam na mikoa ya jirani.

No comments: