WAKIMBIZI 162,156 WA BURUNDI WAPEWA URAIA WA TANZANIA



Rais Jakaya Kikwete ametoa hati za uraia wa Tanzania kwa wakimbizi 162,156 kutoka nchi jirani ya Burundi na ambao wameishi nchini kwa miaka 42, tangu mwaka 1972.
Alitoa hati hizo juzi mjini Tabora, ikiwa nisehemu ya ziara yake ya kikazi ya siku mbili kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo.
Kikwete alitoa hati hizo kwa wakimbizi 19 kwa niaba ya wenzao katika shughuli iliyohudhuriwa na watu mbalimbali akiwemo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe.
Wengine waliohudhuria ni  Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Wakimbizi nchini na Mabalozi wa Uingereza, Canada, Mwakilishi wa Umoja wa Ulaya, Ireland,Ubelgiji na Mwakilishi wa Ubalozi  wa Japan pamoja na Askofu Mkuu, Jimbo Kuu, Kanisa Katoliki la Tabora, Paul Ruzoka wa Jimbo Kuu la Kanisa Katoliki la Tabora..
Shughuli hiyo ilikamilisha mchakato ulioanzishwa na Rais Kikwete mwaka 2007 wakati alipoamua kuwapa wakimbizi hao wa Burundi uraia wa Tanzania baada ya kuwa wameishi nchini kama wakimbizi tangu walipoingia kwa mara ya kwanza mwaka 1972 kutokana na machafuko katika Burundi. Wameishi katika kambi za ukimbizi katika Wilaya ya Kaliua, Mkoa wa Tabora.
Akizungumza katika shughuli hiyo, Mwakilishi wa UNHCR katika Tanzania,  Joyce Mends-Cole alisema Tanzania imekuwa nchi ya kwanza katika historia ya dunia kwa kutoa uraia kwa watu wengi kiasi hicho na kwa wakati mmoja.
Naye Balozi wa Ireland nchini, Fionnula Gilsenan, akizungumza kwa niaba ya Mabalozi wenzake aliisifu Tanzania na kumpongeza Rais Kikwete kwa uamuzi wa kutoa uraia na hati za uraia akisema; “kitendo hiki ni kikubwa na kizuri sana.
“Mheshimiwa Rais umefanya kitu kikubwa mno. Hili ni jambo kubwa na wewe mwenyewe umeshuhudia furaha ya watu hawa. Umesikia nyimbo zao za shukurani kwako na kwa serikali.”
Akizungumza na raia hao wapya wa Tanzania, Rais Kikwete alisema kuwa matarajio yake na yale ya Watanzania ni kuwaomba raia wapya ni kuwaona wakitimiza ahadi yao kwa nchi yao kwa kuwa raia wapya.
“Shughuli hii ni kutimiza tu mchakato kwa sababu hili la uraia wenu tulilimaliza siku nyingi. Matarajio yangu na yale ya Watanzania wenzenu ni nyie kutimiza  ahadi ya kiapo chenu cha kuwa raia wema wa nchi yenu. Heshimuni kiapo chenu.”

No comments: