Wakati hofu
juu ya usalama wa watoto katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam
ikizidi kutanda miongoni mwa wazazi na walezi, Polisi imekanusha kuwapo kwa
matukio ya utekaji nyara watoto wanaosoma shule za msingi na kufanyiwa unyama
ukiwamo ulawiti, kuuawa na hata kuchunwa ngozi.
Kwa wiki
kadhaa sasa, hofu juu ya matukio ya aina hiyo yalichangiwa kwa kiasi kikubwa na
taarifa za mitandao ya kijamii, ikielezea jinsi watoto wanavyotekwa.
Kamanda wa
Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova akizungumza jana,
alisema hivi karibuni umezuka uvumi kutoka kwa watu mbalimbali kwamba lipo
kundi la wahalifu wanaotumia gari aina ya Toyota Noah yenye rangi nyeusi
kutenda uhalifu dhidi ya watoto.
Alisema
Polisi imefanya uchunguzi na mpaka sasa hawana taarifa yoyote ya mtoto kutekwa
au kufanyiwa madhara yoyote kwa mtindo wa utekaji nyara. Kwa mujibu wa kamanda,
polisi inamshikilia mtu mmoja kwa kuhusika kusambaza uvumi huo.
“Polisi
imegundua kwamba huu ni uvumi ambao haujulikani chanzo chake hivyo nawaomba wananchi
kuachana na uvumi huo na kupuuza kwani unaleta hofu katika jamii bila sababu za
msingi na kuleta usumbufu kwa baadhi ya watu,” alisema.
Alisema
Oktoba 3 mwaka huu saa 3.00 asubuhi, Vingunguti, mfanyakazi wa The Guardian
Ltd, Prosper Makame (34) akiwa na mkewe MaryStella Munis (30) mfanyabiashara wa
vyombo vya nyumbani walifika eneo la shule ya msingi Kombo kwa ajili ya
kuchukua fedha za vyombo wakiwa na gari
aina ya Noah yenye namba T 252 DAY rangi nyeusi na kuvamiwa na wananchi.
“Wakati watu
hao wakisubiri kuchukua fedha, ghafla walikuja zaidi ya wananchi 100 na
kuzingira gari hilo huku wakipiga kelele wakidai kwamba ndilo gari linaloteka
wanafunzi. Lakini polisi walipata taarifa hizo mapema na kufika eneo la tukio
na kuwaokoa watu hao pamoja na gari lao,” alisema.
Kova alisema
Oktoba 13 saa 10.00 katika Kituo cha Polisi Tabata katika Manispaa ya Ilala,
uliibuka uvumi kuwa gari namba T 548 BUN aina ya Noah nyeusi ambayo ni mali ya
askari polisi wa kikosi cha Usalama Barabarani, Inspekta Esther lililokuwa
kituoni hapo, ndani yake kulikuwa na vichwa vitano vya watoto wa shule ya
msingi Mtambani.
“Kutokana na
uvumi huo wananchi walikusanyika kituoni hapo ili kushuhudia na kuona hivyo
vichwa vitano, ndipo mkuu wa kituo hicho alipoamuru gari hilo kufunguliwa na
kuwathibitishia wananchi kuwa habari hizo ni za uongo na uvumi,” alisema.
Alisema hali
hiyo ya uvumi ni ya hatari kwa sababu wananchi kila wanapoona Noah nyeusi
wanaikimbilia na kuizingira kwa lengo la kufanya fujo.
“Polisi
tunasisitiza kuwa uvumi huu wa kuwepo kwa kikundi cha wahalifu ambao wamekuwa
wakiwateka watoto na wanafunzi siyo kweli hata kidogo na hivyo wananchi
wanatakiwa kuepukana na taarifa hizo ambazo zinaweza kusababisha uvunjifu wa
amani,” alisema.
Alisema
uchunguzi wa kubaini nani alieneza uvumi huo ulifanyika na kubaini kuwa
umeenezwa na Gilbert Stanley (32), mkazi wa Tabata ambaye alikamatwa.
Alipohojiwa,
kwa mujibu wa kamanda, alikiri kueneza habari hizo na kudai aliambiwa na mtu
mwingine ambaye alidai hamkumbuki.
No comments:
Post a Comment