MUHIMBILI WATENGA SHILINGI MILIONI 80 KWA AJILI YA UTAFITI


Hospitali ya Taifa ya Muhimbili imetenga Sh milioni 80 katika mwaka 2014/2015 kwa ajili ya kufanya utafiti  kwa lengo la kuongeza ubora wa huduma zinazotolewa hospitalini hapo.
Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo, Dk Marina Njelekela wakati wa ufunguzi wa Baraza la Utafiti la hospitali hiyo, ambapo alisema, sambamba na kutengwa kwa fedha hizo pia bodi iliridhia kuanzishwa kwa kitengo cha Mafunzo, Utafiti na Ushauri.
"Leo ni kama tunatimiza eneo la tatu la kuwa na tafiti nyingi, zenye ubora wa juu ambazo zitasaidia katika kuboresha huduma tiba na kinga katika nchi yeti. Hivyo kama hospitali kuu ya taifa tunategemea mwanzo huu mzuri leo utasaidia kufikia azma hiyo," alisema Dk Njelekela.
Alisema hospitali hiyo imekuwa ikitoa nafasi na ushirikiano kwa vyuo vikuu, mashirika na taasisi mbalimbali kufanya tafiti zao katika hospitali hiyo.
Alisema katika majukumu aliyoagizwa moja ni kuhakikisha madaktari na wafanyakazi kutoka maeneo mengine wanaongeza morali ya kufanya tafiti na kuongeza idadi ya tafiti hospitalini hapo.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Baraza la Utafiti na Taifa, Dk Rose Kingamkono ambaye alikuwa mgeni rasmi alisema, baraza hilo litasaidia katika kufanya utafiti na hatimaye kupata suluhisho la magonjwa mbalimbali, ikiwemo yale yasiyoambukizwa ambayo kwa sasa yameongezeka kwa kasi.
Alisema magonjwa yasiyoambukizwa yameongezeka kutokana na mtindo wa maisha wanayoishi watu wengi jambo linalochangia magonjwa hayo. Alisema suala la chakula kwa kiasi kikubwa limesababisha ongezeko la magonjwa hayo.

No comments: