Ni msemo maarufu wa wahenga ambapo Rais wa Zanzibar, Dk Ali
Mohammed Shein aliutumia vilivyo jana katika hotuba yake baada ya yeye na Rais
Jakaya Kikwete kupokea Katiba Inayopendekezwa kutoka kwa Mwenyekiti wa Bunge
Maalumu la Katiba (BMK), Samuel Sitta mjini Dodoma.
Alisema: ‘Hayawi hayawi sasa yamekuwa’ na akaendelea zaidi
kwa kusema: ‘Waliosema hayawezekani sasa yamewezekana’.
Ni maneno ya kiongozi wa ngazi ya juu katika taifa letu na
pia ndiyo maneno ya viongozi wengine na wananchi wapenda amani katika nchi ya
Tanzania baada ya kupatikana kwa Katiba Inayopendekezwa na kukabidhiwa rasmi
kwa viongozi hao wakuu wa nchi kama ilivyokusudiwa kwa sheria na taratibu.
Katika hotuba yake kwenye tukio hilo la kihistoria, Rais
Kikwete alitamka wazi tena kwa furaha kwamba Katiba Inayopendekwezwa
imeandaliwa kwa ubora wa hali ya juu na kusema kuwa kwa kupatikana katiba
inayopendekezwa ajenda ya Watanzania imetimia.
Mapema Mwenyekiti Kamati ya Uandishi, Andrew Chenge aliweka
bayana katika sherehe hiyo kwamba asilimia zipatazo 82 ya mambo yaliyokuwemo
katika rasimu ya Katiba iliyokabidhiwa BMK na Tume ya Mabadiliko ya Katiba
chini ya Jaji mstaafu Joseph Warioba yameingizwa katika Katiba Inayopendekezwa
na asilimia zipatazo 18 tu ndiyo mambo mapya yaliyofanyiwa marekebisho na wajumbe.
Kwa kiwango chochote kile cha ufaulu duniani, hiki ni
kiwango cha hali ya juu na kinastahiki kupongezwa na kila mpenda haki na
maendeleo mema ya kiuchumi, kisiasa, kijamii na kiutamaduni. Ndani ya Katiba
Inayopendekezwa makundi maalumu yakiwemo walemavu, vijana, wanawake, wafugaji,
wavuvi, wachimba madini na mengineyo, yamepewa umuhimu unastahili.
Tuna kila sababu ya kuwapongeza wabunge wote wa BMK waliweza
kufikia hatua hiyo muhimu na ya ngazi ya juu katika mchakato mzima wa kutunga
katiba mpya ya nchi.
Ni ukweli kwamba kuna changamoto nyingi zilizopitiwa hadi
kufikia ngazi hii, lakini yote ni sehemu tu ya mchakato mzima wa kupatikana kwa
katiba nzuri yenye mshiko na maslahi ya taifa.
Kwa hatua hii tuliyofikia, tunapenda kuwashauri Watanzania
wote kwamba sasa ni vema kusahau tofauti zilizokuwapo wakati wa mchakato
uliopita ili kusonga mbele katika hatua itakayofuata ya kuipigia kura ya ndiyo
au hapana, kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo.
Hapa tunapenda kuchukua usemi aliotumia Msanii Mrisho Mpoto
jana wakati anatumbuiza katika sherehe hizo, kwamba ‘Palipoacha kuwasha
usipakune tena.’ Kwa hali ya kawaida kabisa maana yake ni kwamba: ‘Yaliyopita
si ndwele, tugange yajayo.’
Huu sasa ni wakati wa Watanzania kushikamana kwa hali na
mali licha ya tofauti zilizopo, kuhakikisha kwamba wakati wa kupiga kura ya
Katiba Inayopendekezwa, wanashiriki kwa amani, upendo, mshikamano na umoja kama
ilivyo mila na desturi. Mungu ibariki Tanzania.
No comments:
Post a Comment