MKUU WA WILAYA AKAANGWA KWENYE TUME YA MAADILI



Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe, Anna Mwalende ameanika mbele ya Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma ushahidi wake dhidi ya Mkuu wa Wilaya ya Korogwe, Mrisho Gamba na kueleza namna alivyodhalilishwa na kunyanyaswa pamoja na viongozi wengine.
Mwalende ambaye ni shahidi wa tatu katika shauri linalomkabili Gamba, alidai  amefanya kazi serikalini kwa miaka 24 katika utumishi wa umma, miaka saba katika Serikali Kuu na miaka 14 katika halmashauri, lakini miezi mitano aliyofanya katika wilaya hiyo hataisahau maisha yote.
Alikuwa akitoa ushahidi wa upande wa mashtaka ambao ni  Sekretarieti ya Maadili kwa viongozi wa umma,  katika  Baraza la Maadili wa viongozi wa Umma lililo chini ya Mwenyekiti wake, Jaji mstaafu Hamisi Msumi kuhusu tuhuma zinazomkabili DC huyo za kutumia madaraka yake  vibaya alidai kudhalilishwa na Gamba.
Alidai Mkuu huyo wa wilayaamekuwa na lugha chafu kwa viongozi wenzake, ana utawala wa mabavu bila kuzingatia kanuni na sharia, jambo ambalo ni kikwazo kwa maendeleo ya wilaya hiyo. Alidai alitukanwa mbele ya Waziri wa Maji kwa kuitwa  mkurugenzi wa hovyo.
Aidha, alisema mkuu huyo wa wilaya amesababisha kukwama kwa maendeleo ya wilaya hiyo huku akiwaweka `mahabusu’ viongozi wanaofanya kazi kwa kufuata kanuni na sheria kwa kutaka kufuata maamuzi yake.
Mkurugenzi huyo ambaye amesimamishwa kazi na DC huyo na kumleta mkurugenzi mwingine ameeleza kuwa halmashauri hiyo ina wakurugenzi wawili wanaolipwa mishahara hivyo, kuongezea gharama serikali.
Alidai amesimamishwa kazi na mkuu huyo wa wilaya huku tuhuma zikiwa hazijathibitika na kupelekwa mkurugenzi mwingine, hivyo kuwa wawili na wote wanalipwa sawa.
Alidai kwa wakati tofauti amekuwa akimtukana Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo kuwa mwizi na mla rushwa, ikiwa ni pamoja na kuwaambia mmoja wa watendaji wa halmashauri hiyo kuwa amepata shahada kwa kutumia nguo ya ndani.
Alidai kuwa  alipotaka kutekeleza majukumu ya kumwajibisha mfanyakazi mbadhirifu  aliyekuta ripoti yake wakati anaripoti ofisini hapo baada ya tume iliyoundwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) kumuagiza, alimwambia suala hilo litamtokea puani.
“Kuna siku alituita mimi na Ofisa Utumishi na kutaka kumrejesha kazini mwalimu aliyekuwa hajahudhuria kazini kwa miaka mitatu tukakataa ndipo akaagiza tuwekwe rumande, lakini mimi nilikataa na kupewa askari wa kike anilazimishe lakini niliwasiliana na RCO (Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa) sikulala rumande,” alisema.
Alidai kuwa Ofisa Utumishi alilala ndani kwa siku kadhaa na yeye kufuatilia polisi, lakini aliambiwa hawezi kutoka mpaka kwa amri ya DC na baadaye diwani mmoja alifanikiwa kumtoa.
Alidai pia kuwa DC huyo alimweka ndani Mhandisi wa Maji wa wilaya na kutaka achukuliwe hatua na polisi hawakutaka kumtoa mpaka DC alipotoa kibali.
Mkurugenzi huyo alisema amefanya kazi serikalini kwa miaka 24 katika utumishi wa umma, miaka saba katika Serikali Kuu na miaka 14 katika halmashauri, lakini miezi mitano aliyofanya katika wilaya hiyo hataisahau maisha yote.
Baraza lilimtaka kuwasilisha vielelezo vya ushahidi wa sauti zenye maneno ya matusi na maandishi ya uongozi wa mabavu ambayo shahidi huyo alikiri kuwa navyo.
Awali, shahidi wa pili katika shauri hilo, diwani wa Kata ya Mndolwa wilaya ya Korogwe, Hillary Ngonyani ambaye aliwahi kuwa Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo alidai DC huyo aliwahi kumwita `sisimizi’ wakiwa katika vikao vya halmashauri.
Pia aliunga mkono suala la DC huyo kumuita mtumishi mwenzao kuwa amepata shahada kwa kutumia nguo ya ndani na kesi ipo mahakamani huku akiwa na dharau, kiburi, kashfa na kufanya kazi kinyume cha taratibu.
“DC huyu akijua kuwa yeye ni kiongozi amekuwa na dharau na kudhalilisha viongozi wenzake kwa kuwatukana wale wote wanaofanya kazi kwa kuzingatia kanuni na taratibu na kukataa kutii maamuzi yake ambayo ni kinyume,” alisisitiza.
Kutokana na kumpa muda wa kuwasilisha vielelezo shahidi wa tatu, shauri hilo liliahirishwa mpaka kikao cha baraza kijacho ambapo vielelezo vitakuwa vimepatikana.
Wakati huo huo, baraza hilo lilisikiliza mashauri dhidi ya madiwani watano wakiwemo wanne wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambao wanadaiwa kutowasilisha tamko la mali na madeni kwa mujibu wa sheria.
Waliotuhumiwa ni Diwani wa Magomeni, Julian Bujugo (CCM) aliyekiri kutowasilisha tamko hilo mwaka 2012 kutokana na kuwa mbali na mkoa yaliyosababishwa na kufiwa na mke wake, Diwani wa Kata ya Kijitonyama, Uoleuole Juma (Chadema) ambaye kesi ya Uchaguzi bado iko mahakamani.
Wengine ni Diwani wa Kata ya Kunduchi, Janeth Rite (Chadema) aliyedai kupeleka fomu hizo, lakini akashangaa kuambiwa hazijafika, Diwani wa kata ya Sinza Renatus Pamba ambaye alisema amewasilisha tamko na nakala anazo, lakini shauri lake halikukamilika baada ya Mwenyekiti kubaini wanaapa bila kutumia vitabu vya dini.
Jaji Msumi alilalamika kutopelekwa kwa Biblia na Kurani kwa ajili ya kuapa na kusema viapo vyote havikuwa halali na kuahirisha mashauri yaliyobaki hadi leo.

No comments: