MFUMUKO WA BEI WASHUKA MWEZI SEPTEMBA


Mfumuko wa bei wa Taifa kwa mwezi Septemba umepungua hadi asilimia 6.6 kutoka asilimia 6.7 ilivyokuwa Agosti mwaka huu.
Mkurugenzi wa Takwimu za Jamii na Sensa ya Watu na Makazi, Ephraimu Kwesigabo alisema kupungua kwa mfumuko huo wa bei kunamaanisha  kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia Septemba imepungua ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo kwa mwaka ulioishia mwezi Agosti mwaka huu.
Alisema pia kuwa fahirisi za bei zimeongezeka hadi 149.93 mwezi Septemba mwaka huu kutoka 140.1 mwezi Septemba mwaka jana.
Alisema mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi umepungua hadi asilimia 8.5 mwezi Septemba mwaka huu kutoka asilimia 8.8 ilivyokuwa mwezi Agosti mwaka huu.
Kwesigabo alisema kupungua kwa mfumuko wa bei wa mwezi Septemba mwaka huu, kumechangiwa na kupungua kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula kwa kipindi cha mwezi Septemba.
Alisema bei za vyakula zilizoonesha kupungua kwa mwezi Septemba ni pamoja na mchele, ulezi, mahindi, matunda na sukari kwa asilimia 3.5. Alisema bidhaa zisizo za vyakula zilizoonesha kupungua kwa bei mwezi Septemba 2014 ni sare za shule, simu za mkononi, runinga na viatu.
Kwesigabo alisema mfumuko wa bei una mwelekeo unaofanana na nchi nyingine za Afrika Mashariki. Alisema Kenya mfumuko umepungua hadi asilimia 6.6 mwezi Septemba kutoka asilimia 8.36 wakati Uganda mfumuko umefikai asilimia 1.4 kutoka asilimia 2.8.
Kuhusu thamani ya shilingi, Kwesigabo alisema uwezo wa Sh 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma umefikia Sh 66 na senti 70 mwezi Septemba 2014 kutoka mwezi Septemba 2010.

No comments: