MDAHALO WA KUMKUMBUKA NYERERE KUFANYIKA MAKUMBUSHO


Taasisi ya Mwalimu Nyerere kwa kushirikiana na Makumbusho ya Taifa na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) wameandaa maonesho na mdahalo wa kukumbuka na kuenzi mchango wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere katika kujenga, kutetea, kulinda na kudumisha amani.
Maonesho hayo ya siku tano ambayo yatafunguliwa Jumatatu na kumalizika Oktoba 17 yatafanyika katika ukumbi wa Makumbusho ya Taifa yaliyopo jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana ilisema maonesho hayo yatajikita zaidi kuonesha picha, nyaraka, vitabu, matukio na kazi mbalimbali zinazohusu Baba wa Taifa ambaye ni Rais wa Kwanza na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama ya Tanzania.
Mada zitakazotolewa katika mdahalo utakaofanyika tarehe 17 ambayo  ndiyo siku ya kilele  cha makumbusho hayo ni misingi, utekelezaji na usimamizi wa kujenga, kulinda na kudumisha amani na uchambuzi na mifano halisi ya Sera za utekelezaji wa misingi ya kujenga amani kwenye Sekta mbalimbali za maendeleo.
“Lengo kuu la maonesho na mdahalo huo ni kuwawezesha watanzania na hasa vijana kujifunza na kujua misingi ambayo Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere aliizingatia katika kujenga, kutetea, kulinda na kusimamia ili Tanzania iwe nchi ya amani kama ilivyo leo  na pia mchango wake alioutoa  kudumisha amani”.
Baadhi ya misingi mikuu aliyoizingatia ni utu, usawa, haki na heshima kwa binadamu wote. Misingi hii iliifanya Tanzania iwe kitovu na mbeleko ya harakati za ukombozi wa Bara la Afrika na utetezi wa haki za wanyonge duniani”, ilisema Taarifa hiyo.
Maonesho na mdahalo huo vimeandaliwa ili viwe sehemu ya maadhimisho ya miaka 15 tangu kifo cha Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere kilipotokea tarehe Oktoba 14, 1999 katika Hospitali ya Mtakatifu Thomas mjini London nchini Uingereza.
Maadhimisho hayo kitaifa yanafanyika mkoani Tabora.

No comments: