MADAKTARI WA TANZANIA KUTOA HUDUMA YA EBOLA AFRIKA MAGHARIBI


Madaktari  wataalamu watano wa afya wamejitolea kwenda kutoa huduma katika baadhi ya nchi za Afrika Magharibi zilizoathiriwa na ugonjwa wa ebola.
Wataalamu hao walioondoka jana, baadhi yao walizungumza na waandishi wa habari katika mkutano kati ya Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Donan Mmbando na vyombo vya habari.
Dk Mmbando (pichani) aliwataja kuwa ni Dk Justin Maeda kutoka Mvomero, Dk Herilinda Temba kutoka Hospitali ya Mkoa wa Morogoro, Shaban Sasita, Godbless Lucas na mtaalamu wa magonjwa ya mlipuko kutoka Lindi, Theophil Malibiche.
Kwa mujibu wa Dk Mmbando, baada ya kuondoka jana, wamekwenda Ethiopia  ambako watapangiwa majukumu kwa ajili ya kusaidia kukabili  tatizo hilo.
Alisema wataalamu hao watafanya kazi kwa wiki tatu za awali na serikali itaendelea kuwasaidia kutimiza majukumu yao.
Akizungumzia mchakato wa kupata wataalamu hao, alisema walitangaza na baadae wakajitokeza hao ambao wamechaguliwa kwa ajili ya kwenda kujumuika na wataalamu wengine kutoa huduma katika nchi hizo zilizoathiriwa na ebola.
Akizungumza na waandishi wa habari, mmoja wa madaktari hao, Dk Meeda alisema atakubali kukabiliana na hali yoyote katika kazi yake.
Alisema hiyo ni sehemu ya kupata uzoefu hatimaye atakaporudi nchini, asaidie Watanzania endapo ugonjwa huo utajitokeza.
Daktari mwingine, Dk Temba alisema ana moyo wa kusaidia wengine na ndiyo maana ameamua kujitolea kwenda kuhudumia waathirika wa ugonjwa huo.
Awali, Dk Mmbando alisema ebola imekumba zaidi nchi za Afrika Magharibi ambapo hadi sasa takwimu zinaonesha  watu 7,500 wameugua ugonjwa huo.
“Watu 3,500 wamepoteza maisha kutokana na ebola. Ugonjwa huu pamoja na kuwapata wananchi pia umegusa wataalamu wa afya na hauchagui,” alisema Mganga Mkuu.
Aidha alisema, kwa upande wa hapa nchini, wanaendelea na mikakati ya kupambana na ugonjwa huo kama utajitokeza.
Alisisitiza ipo kamati ya kitaifa  ambayo wanakutana kila wiki sanjari na kutekeleza mpango katika ngazi mbalimbali nchini.
Kwa mujibu wa Mganga Mkuu, wizara imetoa mafunzo jinsi ya kuhudumia wagonjwa wa ebola. Hatua hiyo imekwenda sanjari na kutenga kituo maaluma Temeke, jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa wa ebola.
Katika maeneo ya mipakani na viwanja vya ndege vimewekwa vifaa maalumu kwa ajili ya kupima joto la mwili kama lipo juu. Alisisitiza kinachopimwa siyo ebola kwa sababu ugonjwa huo unapimwa katika maabara zilizopatiwa ithibati.

No comments: