Wakati Serikali ikipambana kuhakikisha wimbi la wanafunzi
wanaomaliza kidato cha sita nchini, wanapata fursa ya kujiunga na elimu ya juu,
wanafunzi 9,649 wenye sifa ya kupata mikopo
ili wajiunge na elimu ya juu mwaka huu, wamekosa fursa hiyo.
Juzi Waziri Mkuu, Mizengo Pinda alielezwa kuwa Mradi wa
Sayansi na Teknolojia ya Elimu ya Juu (STHEP) unaosimamiwa na Serikali,
umesaidia kuongeza idadi ya wahadhiri wa ngazi ya Shahada ya Uzamivu (Phd) 79
katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na katika Chuo Kikuu Huria (OUT).
Kati ya wahadhiri hao 79, waliopata udhamini wa kusomea
shahada ya uzamivu, wahadhiri 12 ni kutoka Chuo Kikuu Huria na wahadhiri 67 ni kutoka Chuo Kikuu cha Dar
es Salaam.
Wakati Waziri Mkuu akipata taarifa hizo za maendeleo ya
mradi huo, Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), ilitoa taarifa
jana ikieleza kuwa wanafunzi 9,649 wamekosa mikopo ingawa wana sifa.
Akizungumza kuhusu mradi huo baada ya kufanya ukaguzi wa
utekelezaji wake katika vyuo hivyo juzi, Pinda alisema lengo lake ni kujenga
uwezo wa wataalamu kufundisha wanafunzi wanaomaliza kidato cha sita, ambao kwa
sasa ni wengi.
“Mradi huu ni wa
miaka mitano ambao ulianza mwaka 2009 na unakamilika mwaka huu. Lengo hasa ni
kujenga uwezo wa wataalamu wetu ambao watakuja kufundisha watoto wa kidato cha
sita ambao idadi yao inazidi kuongezeka kila mwaka,” alisema Pinda.
Alisema katika kukabiliana na tatizo la sasa la ongezeko
la wanafunzi wanaomaliza kidato cha sita, Serikali iliamua kukopa fedha kutoka
Benki ya Dunia (WB), ili kuboresha miundombinu kwenye taasisi za elimu ya juu
nchini.
Kwa mujibu wa Pinda, Serikali iliridhia pia fedha hizo
zitumike kujenga miundombinu mipya ya kufundishia pamoja na kukarabati baadhi
ya zamani kwani kama miundombinu haipo, kazi ya kufundisha haitakuwepo.
“Tulikubaliana pia fedha hizo zinunue vifaa kwa maana ya
kompyuta, vifaa vya maabara pamoja na samani za maktaba na baadhi ya madarasa.
Ni fedha za mkopo lakini zimetumika kusaidia Watanzania wote,” alisema.
Akiwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Pinda alikagua
majengo mapya ya ghorofa, ikiwemo jengo la Shule Kuu ya Elimu, Sayansi ya
Majini ambalo litakuwa na kituo cha wanafunzi. Pia alizindua jengo jipya la
Uhandisi Migodi na Usindikaji Madini katika Chuo Kikuu Kishiriki cha Uhandisi
na Teknolojia.
Akitoa taarifa ya miradi yote hiyo, Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Rwekaza Mukandala, alisema katika awamu ya
kwanza ya STHEP, chuo hicho kilipata Sh bilioni 67.
Profesa Mukandala alisema chuo kimefanikiwa kuendeleza
kimasomo wafanyakazi wake zaidi ya 150, kujenga majengo mapya manane, kusomesha
wahadhiri tarajiwa 163 ambapo 63 wamesoma shahada za uzamili na 67 wamepata shahada za uzamivu (PhD).
“Tumenunua vifaa mbalimbali vikiwemo vya maabara,
kompyuta 864, vitabu zaidi ya 960, na vifaa vya teknolojia, uhandisi na
sayansi. Pia tumepanua madarasa, maabara na ofisi.
“Tumepata maabara
mpya 49 zitakazotumiwa na wanafunzi 3,630 kwa wakati mmoja; madarasa 53 yenye
uwezo wa kubeba wanafunzi 4,200 kwa wakati mmoja; ofisi 322 zitakatumiwa na
wafanyakazi wasiopungua 600,” aliongeza.
Akiwa katika Chuo Kikuu Huria, ambako alizindua jengo la
ghorofa 10 lililopewa jina la Open
Distance Learning Tower (ODL Tower)
lililogharimu Sh bilioni 3, Pinda alielezwa kuwa chuo hicho kimesomesha
wahadhiri 29, kati ya 12 wamepata shahada za uzamivu na 17 shahada za uzamili.
Chuo hicho pia kimejenga maabara za kompyuta tatu,
maktaba ya kuweka watu 224 kwa wakati mmoja, vyumba vya mihadhara maabara ya lugha na kununua kompyuta na
samani zingine.
Wakati vyuo vikuu vikifanya maboresho hayo kujiandaa kupokea wanafunzi
wengi zaidi wa elimu ya juu, taarifa ya Kitengo cha Habari, Elimu na
Mawasiliano cha HESLB, imeeleza kuwa kati ya waombaji 42,227 waliojaza fomu za
kuomba mkopo kwa usahihi, waombaji 39,793 walikuwa na sifa za kukopeshwa.
Hata hivyo kwa mwaka wa masomo 2014/2015, Bodi hiyo imeeleza kuwa uwezo
wake ni kutoa mkopo kwa wanafunzi 30, 066 tu wa mwaka wa kwanza wanaosoma ndani
ya nchi na wengine 78 wa mwaka wa kwanza wanaosoma nje ya nchi, na hivyo kuacha
wanafunzi 9,649 wenye sifa bila mikopo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, waombaji wanaoendelea na masomo hawakutakiwa
kujaza fomu za maombi ya mikopo hiyo. Aidha, orodha kamili ya waombaji wapya
waliopangiwa mikopo ipo kwenye tovuti ya Bodi ambayo niwww.heslb.go.tz au www.olas.heslb.go.tz
na muombaji anaweza kutafuta jina lake kwa kutumia namba ya mtihani ya kidato
cha nne.
No comments:
Post a Comment