Watu wanne wamekufa na
wengine 14 wamejeruhiwa na kulazwa katika hospitali ya Wilaya ya Mpanda
baada ya basi la Kampuni ya AN kugongana uso kwa uso na gari jingine.
Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Katavi, Dhahiri Kidavashari alisema ajali hiyo
ilitokea jana nyakati za saa tisa
alasiri katika eneo la Mtamba wilaya ya Mlele mkoani humo katika
barabara ya Mpanda - Tabora.
Aliwataja marehemu kuwa ni Emanuel Kavisha, mkazi wa kijiji cha Kasansa
Tarafa ya Mamba wilaya ya Mlele na
mwingine alifahamika kwa jina moja la Mswaya, ambaye ni mkazi wa Tarafa ya
Inyonga wilaya ya Mlele huku marehemu wengine wawili hawajafahamika majina yao.
Alisema ajali hiyo ilihusisha basi
aina Scania mali ya Kampuni ya AN yenye namba za usajili T 502 ALG nililokuwa
likitokea Tabora kuelekea Mpanda na
Costa yenye namba za usajili T 970 ASJ mali ya Emoro, mkazi wa Kerema Wilaya ya
Mpanda, lililokuwa likiendeshwa na Abdu Feruzi likiwa linatokea Mpanda
mjini kwenda Tabora.
Aliwataja majeruhi waliolazwa katika hospitali ya Wilaya ya Mpanda kuwa ni
Jafari Jackison, Leonald Patrick (26)
David Linus (25), Donald Gabriel (43) Nicolas Wilaamu (25) wote wakazi wa tarafa ya Inyonga Wilaya
ya Mlele.
Wengine ni Christopher Kapaya ,
Jackson Shila (15), Joseph Chalula (16) wakazi wa Wilaya ya Nkasi, Rukwa ambapo
majeruhi wote wamelazwa katika hospitali ya Wilaya ya Mpanda.
Kidavashari alisema chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa magari hayo na
dereva wa Costa alikimbia mara baada ya kutokea kwa ajali hiyo na jeshi la
polisi linaendelea kumsaka.
Kwa upande wake, Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Mpanda, Dk Jafari
Kitambwa alisema hali ya majeruhi waliolazwa hospitalini hapo inaendelea
vizuri.
No comments:
Post a Comment