Mbunge wa Ismani na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu
(Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi amemtaka Katibu Mkuu wa Chama Cha
Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana kuhoji utendaji kazi wa Waziri wa Maliasili
na Utalii, Lazaro Nyalandu.
Ombi la Lukuvi kwa Kinana linatokana na kile alichosema ni
kitendo cha waziri huyo kutojibu barua mbili alizoandikiwa na Mkuu wa Mkoa wa
Iringa, Dk Christine Ishengoma kuhusu
malalamiko ya wananchi dhidi ya mwekezaji wa kampuni ya utalii wa
uwindaji ya Kilombero North Safaris.
“Wananchi walikuja kwangu mara mbili kule Dodoma kuhusu
hili. Kuna barua mbili zimeandikwa kwa (Lazaro) Nyalandu na Mkuu wa Mkoa
(Ishengoma) ambazo mimi nimetuma tena nakala zake mara tatu, lakini hakuna
majibu yaliyotolewa,” alisema Lukuvi.
Aliendelea kusema; “Ukifika Dar es Salaam utuite pamoja na
Nyalandu, nadhani wewe (Kinana) ukimwita utamfundisha kuwa viongozi wenzako
wakikuandika, lazima ujibu.
“Najua huko atasema namshitaki lakini mimi ndio co-ordinator
(mratibu) wa Serikali nasema yaliyo ya kweli,” alisema na kuongeza: “ Kama mkuu
wa mkoa anaandika barua, halafu hajibu, haifai.”
Kwa mujibu wa Lukuvi, barua ya kwanza ni ya wananchi
walioomba eneo la Lunda Mkwambi liondoshwe kama eneo la hifadhi na kuwa la
ufugaji ambao wana uwezo wa kuchunga mifugo yao huku wakiwa walinzi wa wanyama.
Lukuvi alisema barua ya pili ni ya kumtaka Waziri Nyalandu
kuingilia kati mgogoro kati ya Jumuiya ya Mbomipa na mwekezaji Kilombero North
Safaris.
Alisema pamoja na viongozi wa Mbomipa, ‘kula bila kunawa’
katika kuingia mkataba huo, lakini waliokula zaidi ni watu wa wizara kwa sababu
hakuna mkataba unaoingiwa bila wizara ya maliasili kufahamu.
“Wizara ya Maliasili na Utalii imehusika na kuwaingiza
mkenge hawa watu wa Mbomipa,” alisema.
Awali, Mkazi wa Kijiji cha Idodi, Danny Salum alimwomba
Katibu Mkuu Kinana kumwondoa mwekezaji Kilombero North Safari kwa kile
alichodai ameshindwa kutekeleza ahadi zake za kutoa mapato, kujenga hoteli ya
kisasa na kambi.
Alisema mwaka 2008, Mbomipa inayoundwa na vijiji 21 vya
tarafa ya Pawaga na Idodi, vinavyozunguka Hifadhi ya Taifa ya Ruaha, iliingia
mkataba wa miaka 25 na mwekezaji huyo.
Alisema ikiwa ni zaidi ya miaka mitano imepita tangu
mwekezaji huyo aanze kazi zake za uwindaji, vijiji vya jumuia hiyo
havijanufaika .
Salum alisema kabla ya uwekezaji huo, jumuia hiyo ilikuwa
ikipata mapato ya kati ya Sh milioni 200 na 300 kwa mwaka hivyo kufanya kila
kijiji kupata mgawo wa Sh milioni 2.4 kila mwaka kwa ajili ya kufanya maendeleo
na ulinzi.
Alisema kupitia fedha hizo walikuwa na uwezo wa kusomesha
watoto wawili waliofaulu katika kila kijiji hivyo kufanya kila mwaka kusomesha
wanafunzi 44.
Kwa mujibu wa mwanakijiji huyo, kutokana na mwekezaji huyo
kutotoa mapato kwa vijiji, wamepoteza fursa za kusomesha watoto 210 wanaoingia
kidato cha kwanza.
Vijiji vinavyounda Mbomipa ni Idodi, Ilolompya, Isele,
Kinyika, Kisanga, Luganga, Mafuluto, Magozi, Mahuninga, Makifu, Mboliboli,
Mkombilenga, Nyamahana, Itunundu, Kimande, Malizanga, Mbuyuni, Mapogoro, Kitisi
na Magombwe.
Kinana aliahidi kushughulikia jambo hilo akisema: “Mkuu wa
mkoa naomba nakala za barua mlizoziandika ili tukaulizane kwa nini waziri
ukiandikiwa barua hujibu. Hii Serikali siyo mali mtu bali ni ya wananchi,
lazima ajibu.”
Alisema tabia ya kujibu barua serikalini bado iko hovyo.
Alikumbusha watumishi wa serikali kuwa utumishi serikalini ni wa wananchi kwa
sababu serikali ni ya wananchi.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika
Kata ya Ilola Wilaya ya Iringa Vijijini, Kinana akawataka mawaziri ambao
wameshindwa kutumikia wananchi na kutatua kero zao, wamweleze Rais Jakaya
Kikwete waachie nafasi hizo.
Alikuwa akizungumzia mgogoro wa mipaka kati ya Magereza na
vijiji ambao inadaiwa umeshindwa kutatuliwa na mamlaka husika.
“Hizi kazi tumezikubali za nini? kama kazi imekushinda,
mwandikie bwana mkubwa (Rais Jakaya Kikwete), mwambie siwezi kazi yako. Wa
kuchukua kazi hiyo wako wengi,” alisema.
Alisema pamoja na baadhi ya mawaziri kupelekewa barua za
malalamiko ya migogoro ya wananchi, wanashindwa kwenda vijijini kutatua
matatizo hayo, wakati ni wa kwanza kwenda Ulaya wanapopata mialiko ya huko.
“Leo hii mawaziri
wakipewa barua ya mwaliko kwenda Ulaya wa kwanza kwenda, akiandikiwa barua na
Mkuu wa Mkoa kuwa wananchi wana mgogoro wa ardhi njoo, haji. Utasikia mbali,
jua, vumbi, upepo,” alisema Kinana.
Aliongeza: “Anaandikiwa barua tatu na mkuu wa mkoa haji,
hebu muulize amekwenda Ulaya mara ngapi tena wakati mwingine kwa mikutano ya
porojo ambayo haina tija. Tutakwenda kushikana mashati.”
Kinana alisema viongozi hao wanatakiwa kujua kuwa kuna
Watanzania ambao wako tayari kuwatumikia wananchi kwa hela ndogo
Alitolea mfano wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba waliotaka
waongezewa posho za vikao kutoka Sh 300,000 hadi Sh 700,000 kwa siku wakati
wapo walimu waliibuka na kumwambia Waziri Mkuu, Mizengo Pinda wako tayari
kufanya kazi hiyo kwa Sh 40,000 kila siku.
Awali mwananchi kutoka Kisanga alimwomba Kinana kusaidia
kutatua tatizo la mpaka kati ya kijiji hicho na Magereza ya Pawaga ambao
umedumu kwa zaidi ya miaka sita.
Pia Mbunge wa Ismani, Lukuvi aliwataka wananchi hao kuacha
kupoteza nauli kwenda kushughulikia suala hilo na kuwataka kuendelea kulima
mpaka hapo wahusika watakapoona umuhimu wa kupima mipaka.
“Nimeshamwambia kamishna kuwa nimeshaamua, wananchi wa
Kisanga wataendelea kulima eneo lile, haki ya ardhi ni ya yule anayelima sasa,
mimi nipo na mwakani mtaendelea kulima mpaka hapo watakapozinduka na kuja
kupima,” alisema.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Dk Ishengoma alisema walifanikiwa
kutatua mgogoro wa vijiji vya Itunundu na Mbolimboli na kuwa mpaka wa Kisanga
uliwawia vigumu hivyo kumwandikia barua Waziri wa Mambo ya Ndani, aliyeelekeza
kuwa Kamishina wa Magereza angefika kutatua tatizo hilo.
“Kamishina aliwahikufika hapa Iringa kwa shughuli zingine
lakini hakuweza kufika katika eneo la mgogoro, hivyo mkoa bado unaendelea
kufuatilia,” alisema.
Chanzo cha mgogoro ni gereza kupima na kuweka alama ya
mipaka katika eneo la gereza ambalo vijiji vya Itunundu, Mbolimboli na Kisanga
vilijikuta vikiwa ndani ya eneo la Gereza.
No comments:
Post a Comment