Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa
Umma, Celina Kombani ametoa msaada muhimu wa Sh milioni 40 na bati 300 kwa
ajili ya kukamilisha ujenzi wa vyumba vya maabara katika shule 12 za sekondari
zilizopo katika jimbo la Ulanga Mashariki wilayani humo, mkoani Morogoro.
Mbali na msaada huo pia amesaidia vifaa mbalimbali
ikiwamo sare, viatu na vyakula vyenye thamani ya Sh milioni 7.2 kwa askari wa
jeshi la Mgambo wa wilaya ambao wanatumika kufyatua matofali kwa ajili ya
kukamilisha ujenzi wa vyumba vya maabara.
Kombani ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Ulanga Mashariki
alikabidhi misaada hiyo kwenye ziara yake aliyoianza jimboni humo jana, ambapo
alisema ameamua kusaidia ujenzi huo wa maabara ili jimbo la Ulanga Mashariki
liweze kutoa wanafunzi wenye utaalamu wa masomo ya sayansi katika siku za
usoni.
Kutolewa kwa msaada huo kwa wilaya hiyo kunaweza
kufanikisha utekelezaji wa agizo la Rais Jakaya Kikwete alilolitoa kwa wakuu wa
wilaya, wakurugenzi wa halmashauri na wakuu wa mikoa wawe wamekamilisha ujenzi
wa vyumba vitatu vya maabara kila shule ya sekondari ya kata ifikapo Novemba
mwaka huu.
Kwa mujibu wa agizo la Rais, kiongozi yeyote katika ngazi
za wilaya na mkoa kote nchini atakayeshindwa kutimiza wajibu kwa kutekeleza
agizo hilo, atachukua maamuzi magumu dhidi yake.
Hata hivyo alisema, ili kufikia muda uliopangwa wa
kukamilika kwa maabara hizo wameamua kuwatumia askari wa mgambo kwa ajili ya
kutengeneza matofali na ujenzi huo, ikiwa ni sehemu ya mchango wao katika
kuleta maendeleo.
“Mimi nilishaanza kwa baadhi ya shule za jimboni
mwangu kujenga vyumba vya maabara kabla
ya agizo la rais, kwa hiyo huu ni
mwendelezo na nia yangu ni kuhakikisha wana Ulanga wanasoma masomo ya sayansi
kwa vitendo kwani dunia ya sasa ni sayansi na teknolojia,” alibainisha Waziri
Kombani.
Hata hivyo alitumia fursa hiyo kwa kusema katika mafunzo
yajayo ya mgambo atajitahidi
kuwapeleka wakufunzi wa masuala
ya ujasilimali ili wakati wanapata mafunzo pia wafundishwe namna ya kuendesha
ujasilimali na sio ulinzi pekee ili waweze kujikwamua kwa kuongeza kipato.
Kwa upande wake,
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Isabela Chilumba, alisema ujenzi wa vyumba vya maabara unaendelea na
wananchi wameshahamasishwa kupitia mikutano mbalimbali kwa ajili ya kuchangia
chochote ili kukamilisha ujenzi huo.
No comments:
Post a Comment