Uongozi wa Bunge Maalumu la Katiba, umemuagiza Mpigachapa Mkuu wa Serikali, kupiga chapa upya Katiba Inayopendekezwa, baada ya kubaini makosa ya uchapaji, ikiwemo kuandikwa kwa makosa kwa mjumbe wa bunge hilo kupitia NCCR-Mageuzi Zanzibar, Haji Ambar Khamis.
Katika chapisho la
Katiba Inayopendekezwa, mjumbe Khamis ameonekana kama vile alishiriki katika
awamu ya pili ya Bunge Maalumu la Katiba, wakati hakushiriki.
Kosa hilo na mengine ya
uchapaji, yamekuwa yakitumika kwa makusudi kupotosha umma kuwa Katiba
Inayopendekezwa, ilipita katika mazingira ya kuchakachua kura za wajumbe, ili
kuiondolea uhalali wake wakati wa kupiga kura ya maoni.
Moja ya jitihada hizo ni
pamoja na hatua ya mjumbe Khamis, kuangua kilio juzi mbele ya waandishi wa
habari na kukimbizwa hospitalini kwa matibabu, baada ya kukiri chini ya kiapo
cha chama chake cha NCCR-Mageuzi, kuwa hakushiriki kuipitisha Katiba
Inayopendekezwa.
Akizungumza na mwandishi jana katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam,
Naibu Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, Dk Thomas Kashililah, alisema jina la
Khamis kuwepo katika orodha hiyo, ni moja kati ya makosa kadhaa yaliyobainika.
“Sisi tulibaini kasoro
hiyo na mengine ya uchapaji siku ya kukabidhi Katiba hiyo Pendekezwa na
kuelekeza Katiba hiyo ichapishwe upya baada ya kufanyiwa marekebisho,” alisema
Dk Kashililah.
Alifafanua kuwa kuna
vitabu vya aina mbili, kimoja kinachotumika kwa ajili ya kumbukumbu, ambacho
kina majina ya wajumbe wote wa Bunge Maalumu la Katiba, wakiwemo wajumbe wa
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na wajumbe wengine ambao si wa Ukawa,
lakini hawakushiriki kupiga kura.
Kitabu cha pili kwa
mujibu Dk Kashililah, kimeorodhesha majina ya washiriki wa Bunge hilo katika
awamu zote, ambacho wajumbe wa Ukawa na wengine ambao si wa kundi hilo hawapo
kwa kuwa hawakushiriki mpaka mwisho.
“Baada ya kurekebisha
(kile kitabu cha kumbukumbu) ili kupata
kitabu kinachoeleza wajumbe waliopitisha Katiba Inayopendekezwa, jina
hilo lilipita kimakosa wakati hakupiga kura, tunathibitisha hilo kosa kwa kuwa
ni kweli hakuwepo kupitisha Katiba hiyo,” alisema.
Alifafanua kuwa katika
orodha ya wapigakura, Mjumbe huyo wa NCCR-Mageuzi, alikuwa namba 63 lakini
hakupigakura jambo ambalo haliathiri hata kidogo kura zilizopitisha Katiba
Inayopendekezwa.
Pia Dk Kashililah alitoa
ufafanuzi kuhusu wajumbe waliopiga kura kwa kusema jumla walikuwa 631, lakini
baada ya mmoja kufariki walibaki 630 na kati yao, 411 walikuwa wa Tanzania Bara
na 219 wa Zanzibar.
Alisema idadi hiyo
ilipatikana baada ya mjumbe Salim Suleiman Ally kuondolewa Zanzibar na kuwekwa
upande wa Tanzania Bara baada ya kuwekwa Zanzibar kimakosa.
Katika upande wa
Zanzibar theluthi mbili ya kura zilizotakiwa kupitisha Katiba Inayopendekezwa,
zilipaswa kuwa 146, hata hivyo Katiba hiyo kila ibara ilipitishwa kwa wastani
wa kura 146 na 148.
Kwa upande wa Tanzania
Bara, wajumbe 335 walipiga kura ambapo kila ibara ilipata wastani wa kura 331
mpaka 334, na hivyo kuzidi theluthi mbili iliyokuwa ikihitajika ya 274.
Katika hatua nyingine,
Rais Jakaya Kikwete, amewataka Watanzania kupuuza watu wachache wanaodai kuwa
Katiba Inayopendekezwa ni mbaya, na badala yake wajiandae kuipigia kura ya
kuikubali wakati ukiwadia.
Rais Kikwete alitoa
ushauri huo kwa nyakati tofauti juzi kwa wananchi mkoani Mwanza ambako yupo
katika ziara ya kikazi ya siku tatu, kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo.
“Watakuja watu
kuwashawishi kuwa Katiba Inayopendekezwa ni mbaya, wasikilizeni lakini tumieni
akili yenu, kama ile hadithi ya mbayuwayu. Jiandaeni tu kupiga kura na kuunga
mkono Katiba Inayopendekezwa kwa sababu hii ni Katiba nzuri sana,” alisema Rais
Kikwete.
Alishangaa watu wanaodai
kuwa Katiba Inayopendekezwa ni mbaya, akiuliza kuwa kama Katiba hiyo ni mbaya
basi hiyo nzuri ikoje?
Aliisifu Katiba
Inayopendekezwa kwa kujali makundi yote ndani ya jamii na kusisitiza kwamba
kamwe haiwezi kuwa Katiba mbaya.
“Sijui Katiba nyingine
duniani ambayo inajadili makundi yote ndani ya jamii kama hii Katiba
Inayopendekezwa. Hakuna aliyeachwa – wavuvi wamo, wajane wamo, wafanyabiashara
ndogo wamo, akinamama lishe wamo, wakulima wamo, wafungaji wamo….kila mtu yumo.
Akinamama ndio usiseme kabisa wao wamepata hata asilimia 50 kwa 50 ndani ya
Bunge,” alisema Rais Kikwete.
Aliongeza Rais Kikwete: ”Hivi katiba mbaya inakuwa kama
inayopendekezwa na kama hii inayopendekezwa ni mbaya sasa hivi nzuri ikoje?”
No comments:
Post a Comment