KATIBA PENDEKEZWA IMEKOSEWA, SASA KUCHAPISHWA UPYA


Uongozi wa Bunge Maalumu la Katiba, umemuagiza Mpigachapa Mkuu wa Serikali, kupiga chapa upya Katiba Inayopendekezwa, baada ya kubaini makosa ya uchapaji, ikiwemo kuandikwa kwa makosa kwa mjumbe wa bunge hilo kupitia NCCR-Mageuzi Zanzibar, Haji Ambar Khamis.
Katika chapisho la Katiba Inayopendekezwa, mjumbe Khamis ameonekana kama vile alishiriki katika awamu ya pili ya Bunge Maalumu la Katiba, wakati hakushiriki.
Kosa hilo na mengine ya uchapaji, yamekuwa yakitumika kwa makusudi kupotosha umma kuwa Katiba Inayopendekezwa, ilipita katika mazingira ya kuchakachua kura za wajumbe, ili kuiondolea uhalali wake wakati wa kupiga kura ya maoni.
Moja ya jitihada hizo ni pamoja na hatua ya mjumbe Khamis, kuangua kilio juzi mbele ya waandishi wa habari na kukimbizwa hospitalini kwa matibabu, baada ya kukiri chini ya kiapo cha chama chake cha NCCR-Mageuzi, kuwa hakushiriki kuipitisha Katiba Inayopendekezwa. 
Akizungumza na mwandishi jana katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere, Dar es Salaam, Naibu Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, Dk Thomas Kashililah, alisema jina la Khamis kuwepo katika orodha hiyo, ni moja kati ya makosa kadhaa yaliyobainika.
“Sisi tulibaini kasoro hiyo na mengine ya uchapaji siku ya kukabidhi Katiba hiyo Pendekezwa na kuelekeza Katiba hiyo ichapishwe upya baada ya kufanyiwa marekebisho,” alisema Dk Kashililah.
Alifafanua kuwa kuna vitabu vya aina mbili, kimoja kinachotumika kwa ajili ya kumbukumbu, ambacho kina majina ya wajumbe wote wa Bunge Maalumu la Katiba, wakiwemo wajumbe wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) na wajumbe wengine ambao si wa Ukawa, lakini hawakushiriki kupiga kura.
Kitabu cha pili kwa mujibu Dk Kashililah, kimeorodhesha majina ya washiriki wa Bunge hilo katika awamu zote, ambacho wajumbe wa Ukawa na wengine ambao si wa kundi hilo hawapo kwa kuwa hawakushiriki mpaka mwisho.
“Baada ya kurekebisha (kile kitabu cha kumbukumbu) ili kupata  kitabu kinachoeleza wajumbe waliopitisha Katiba Inayopendekezwa, jina hilo lilipita kimakosa wakati hakupiga kura, tunathibitisha hilo kosa kwa kuwa ni kweli hakuwepo kupitisha Katiba hiyo,” alisema.
Alifafanua kuwa katika orodha ya wapigakura, Mjumbe huyo wa NCCR-Mageuzi, alikuwa namba 63 lakini hakupigakura jambo ambalo haliathiri hata kidogo kura zilizopitisha Katiba Inayopendekezwa.
Pia Dk Kashililah alitoa ufafanuzi kuhusu wajumbe waliopiga kura kwa kusema jumla walikuwa 631, lakini baada ya mmoja kufariki walibaki 630 na kati yao, 411 walikuwa wa Tanzania Bara na 219 wa Zanzibar.
Alisema idadi hiyo ilipatikana baada ya mjumbe Salim Suleiman Ally kuondolewa Zanzibar na kuwekwa upande wa Tanzania Bara baada ya kuwekwa Zanzibar kimakosa.
Katika upande wa Zanzibar theluthi mbili ya kura zilizotakiwa kupitisha Katiba Inayopendekezwa, zilipaswa kuwa 146, hata hivyo Katiba hiyo kila ibara ilipitishwa kwa wastani wa kura 146 na  148.
Kwa upande wa Tanzania Bara, wajumbe 335 walipiga kura ambapo kila ibara ilipata wastani wa kura 331 mpaka 334, na hivyo kuzidi theluthi mbili iliyokuwa ikihitajika ya 274.
Katika hatua nyingine, Rais Jakaya Kikwete, amewataka Watanzania kupuuza watu wachache wanaodai kuwa Katiba Inayopendekezwa ni mbaya, na badala yake wajiandae kuipigia kura ya kuikubali wakati ukiwadia.
Rais Kikwete alitoa ushauri huo kwa nyakati tofauti juzi kwa wananchi mkoani Mwanza ambako yupo katika ziara ya kikazi ya siku tatu, kukagua na kuzindua miradi ya maendeleo.
“Watakuja watu kuwashawishi kuwa Katiba Inayopendekezwa ni mbaya, wasikilizeni lakini tumieni akili yenu, kama ile hadithi ya mbayuwayu. Jiandaeni tu kupiga kura na kuunga mkono Katiba Inayopendekezwa kwa sababu hii ni Katiba nzuri sana,” alisema Rais Kikwete.
Alishangaa watu wanaodai kuwa Katiba Inayopendekezwa ni mbaya, akiuliza kuwa kama Katiba hiyo ni mbaya basi hiyo nzuri ikoje?
Aliisifu Katiba Inayopendekezwa kwa kujali makundi yote ndani ya jamii na kusisitiza kwamba kamwe haiwezi kuwa Katiba mbaya.
“Sijui Katiba nyingine duniani ambayo inajadili makundi yote ndani ya jamii kama hii Katiba Inayopendekezwa. Hakuna aliyeachwa – wavuvi wamo, wajane wamo, wafanyabiashara ndogo wamo, akinamama lishe wamo, wakulima wamo, wafungaji wamo….kila mtu yumo. Akinamama ndio usiseme kabisa wao wamepata hata asilimia 50 kwa 50 ndani ya Bunge,” alisema Rais Kikwete.
Aliongeza Rais Kikwete: Hivi katiba mbaya inakuwa kama inayopendekezwa na kama hii inayopendekezwa ni mbaya sasa hivi nzuri ikoje?”

No comments: