HATMA YA KATIBA MPYA MIKONONI MWA MWANASHERIA MKUU


Wakati kukiwa na matamanio na ushauri wa kutaka Rais Jakaya Kikwete kuhakikisha Katiba Mpya inapatikana kabla ya kuondoka madarakani, hatma yake haijafahamika badala yake,  suala hilo imeachwa kwa  Ofisi  ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupatiwa ufumbuzi.
Rais Jakaya Kikwete alisema jana kwamba kwa kuwa  Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2012 inatamka baada ya  Katiba Inayopendekezwa kukabidhiwa, kura ya maoni inatakiwa ifanyike ndani  ya siku 84, jambo ambalo inabidi bunge lijalo lifanye  mabadiliko yatakayowezesha kura ya maoni kufanyika baada ya uchaguzi mkuu.
Kikwete alisema hayo jana kwenye sherehe za kukabidhiwa Katiba Inayopendekezwa zilizofanyika mjini Dodoma iliyokabidhiwa  pamoja na Rais wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein.
Rais ambaye kwenye sherehe hizo alieleza milima na mabonde aliyokumbana nayo katika kuanzisha mchakato wa kutengeneza Katiba Mpya , alisema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba inataka kuendesha kura ya maoni ndani ya siku 84 kutoka tarehe ya rais kupokea katiba inayopendekezwa.
Hata hivyo alisema kulingana na maoni yaliyotokana na mazungumzo kati yake na viongozi wa vyama vinavyounda  Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD), ilibainika muda ulibaki ni finyu na hautawezesha wala kutosha kukamilika kwa shughuli hii kutokana na Tume ya Uchaguzi kutokamilisha mchakato wa daftari la wapiga kura.
Alisema kutokana na maoni hayo, ilikubalika kushughulikia mambo ya msingi ili kuwezesha  uchaguzi kufanyika na  hatimaye  Kura ya Maoni ufanyike baadaye.
“Inabadi sheria hii ipelekwe bunge lijalo kuruhusu mabadiliko hayo. Maanake sasa ni siku 84. Nataka kusema Mwanasheria Mkuu wanaangalia nini kinaweza kufanyika…mchakato unaendelea,” alisema Kikwete.
Aliendelea kusema, “Lakini pia wako watu wanasema tufanye sasa kura ifanyike tumalize (alishangiliwa) lakini tume inasema wao wanaandika daftari jipya na kazi inaisha Mei. Hapo ndipo penye mgogoro. “
Hata hivyo alisema wapo ambao wamekuwa wakimwambia kwamba mbona mbunge akifariki,  uchaguzi hunafanyika na hivyo kuhoji kwa nini daftari linalotumika kwa ajili ya uchaguzi huo mdogo, lisitumike kwa kura ya maoni. “Penye wengi pana mengi.  Haya ndiyo yanaendelea kwenye tafakuri…” ikifika mwisho wananchi watafahamishwa, “ alisema.
Miongoni mwa waliotamka bayana matamanio ya Kura ya Maoni kupigwa kabla ya Rais Kikwete kutoka madarakani, ni pamoja na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda aliyetoa maoni hayo wakati wa kuhitimisha Bunge Maalumu la Katiba .
Kauli hiyo ya Pinda iliyoungwa mkono na watu wengine akiwemo mjumbe wa bunge hilo,  Askofu Amos Mhagache aliyesisitiza jana kwenye sherehe hizo, ilizua mjadala huku baadhi ya watu wakiitafsiri kana kwamba ni uamuzi wa Serikali na hivyo kushutumu kuwa inapinganana na makubaliano yaliyofikiwa kwenye.
Rais Kikwete ambaye alisisitiza kwamba tukio hilo la kukabidhiwa Katiba Inayopendekezwa ni muhimu na la kihistoria linalokidhi matakwa ya Sheria,  alisema kukamilika kwake  kunabakiza hatua moja ya mwisho ya wananchi wote kupiga kura ya maoni kufanya uamuzi wa katiba mpya.
 “Tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa hapa tulikofikia,…hakika Mungu anaipenda nchi yetu” alisema na kushukuru u na kumpongeza Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel  Sitta na Makamu wake, Samia Suluhu kwa kazi waliyoifanya pamoja na wajumbe wengine kukamilisha kazi hiyo kwa kiwango cha juu.
Alisema, “haikuwa kazi rahisi hata kidogo, kulikuwa na milima na mabonde, na wakati  mwingine mawimbi ambayo yalikuwa makali yalielekea kuwa tufani.”
Alisema mchakato wa katiba mpya ni jambo o jema aliloanzisha kwa nia njema ingawa lilipokewa kwa hisia tofauti. Alisema wapo walioona kwamba halitawezekana lakini yeye alibaki kuwa mmoja wa walioamini  kwamba litawezekana.
Kwa mujibu wake, Desemba 31, 2010 alipotangaza  dhamira ya kuanza mchakato wa katiba, ilipokewa kwa hisia tofauti;  kwa maana wapo waliunga mkono moja kwa moja, wapo waliopinga na waliobaki katikati.
Alisimulia,  alisema jambo ambalo wengi hawalifahamu, ni kwamba makundi hayo yalikuwepo pia ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Nakumbuka walikuwepo baadhi ya watu waliodiriki hata kulihoji na kuniambia kuwa wewe jambo hili umelizua wapi?...Hii si ajenda ya CCM bali ni ya watu wengine.”
Alisema aliwaambia hiyo ni ajenda ya Watanzania na kwamba yeye ndiye mwaklishi wao mkuu ambaye ana dhamana hiyo. “Nashukuru Mungu baada ya mjadala mkali, tuakelewana,” alisema na kuendelea  kusimulia kwamba, “walikuwepo pia watu walioondoka pale shingo upande wakisema jamaa anaingiza jambo ambalo si letu.
Kwa mujibu wa Rais Kikwte, baadhi ya waliokuwa wakali kwenye NEC na Kamati Kuu ya chama,  aliwateua kuwa wajumbe wa  Bunge Maalumu ambao hata hivyo alisema anafurahi kwamba watu hao wamekuwa msaada mkubwa na kutooa mchango mkubwa uliowezesha bunge kupendekeza katiba iliyo nzuri.
Alisema hatimaye wameelewa hoja na haja ya kuandika katiba mpya ulioanza mwaka 2011 kwa serikali kuandaa Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ambao ulijadiliwa na kupitishwa Novemba 18, 2011.
Changamoto nyingine alizosema ni sintofahamu iliyojitokeza kwenye Bunge ambayo baadhi ya wabunge walisusa wakitaka Rais  asiridhie muswada wa sheria hadi hapo yatakapofanyika marekebisho waliyoona wao ni muhimu.
Wakakubaliana kuwa kila chama kilete mapendekezo ya marekebisho wanayoona yanafaa yafanyike. Wakawa na kamati ya pamoja kati ya serikali na wao wakachambua moja baada ya jingine wakakubaliana kuwasilisha kwenye bunge.
Akizungumzia mara nyingine ya baadhi ya wabunge (Ukawa) kususa, Rais Kikwete wabunge waliobaki na hasa wengi wao wakiwa wa CCM , walikuwa wakimwambia safari hii asikutane nao, awaache kwamba kazi wataifanya na kumaliza bila ya wao.
“Niliwasikiliza lakini nikafanya uamuzi wa kiuongozi; kwamba lazima tufanye jitihada shughuli hii tuifanye wote tuimalize wote,” alisema.
Aidha alisema kutokana na mchakato wa bunge kukumbwa na malumbano ya mara kwa mara, pia alikuwa akishauriwa ikiwemo kupokea meseji nyingi zilizomtaka  avunje Bunge Maalumu la Katiba.
Rais meomba wananchi kupokea katiba inayopendekezwa akisema ni nzuri hana wasiwasi nayo. “Tumefika mahali pa kuanza safari ya uamuzi wa mwisho kwa kupiga kura.”
Alihadharisha wananchi  kwamba wataambiwa mengi kwa kuwa wapo wasemaji wengi.  Aliwakumbusha kuzingatia msemo wa akili za mbayu wayu wa kuchanganya akili za kuambiwa na zao.
Alisema anaamini  Katiba inayopendekezwa inafaa na katiba mpya iliyo nzuri inawezekana.
Alipongeza wajumbe kwa kutendea haki matarajio ya Watanzania na kuwaambia kwamba majina yao yameandikwa kwa dhahabu kwa kutengeneza Katiba inayojumuisha maslahi ya makundi yote na kuyajali.
Alitaja makundi hayo ni pamoja na wafugaji, wakulima, wazee, wanawake.  “Tangu dunia iumbwe, mfugaji hajawahi kutajwa kwenye katiba yoyote ile,” alisema na kuongeza upande wa wanawake kuwa katiba imesisitiza lazima 50 kwa 50 itekelezwe.  Alisema hakuna nchi ya Afrika inayoifikia kwa kuweka suala hilo kwenye katiba.
Katiba imependekeza mgawo mzuri wa mamlaka na madaraka katika muungano. Orodha ya mambo ya muungano ni mpya, yale yote yaliyokuwa yakituletea gozi gozi yameondoka…yamekuwa 16 na siyo 22,” alisema na kusisitiza kwamba mambo yaliyokuwa na kero kubwa upande wa Zanzibari yamepatiwa majawabu.
Alieleza pia kuguswa na uwapo wa sura inayohusu ardhi, maliasili na mazingira ambayo kwa mujibu wake, ndiyo mambo ya msingi ambayo katiba isip0okuwa nayo kuna upungufu mkubwa.
Alisema katiba imekubaliwa kwa theluthi mbili kwa kila upande jambo alilosema halikuwa rahisi hasa kwa upande wa Zanzibar ambayo wajumbe siyo wengi.
Rais Kikwete ambaye alipongeza wadau mbalimbali ikiwemo Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Warioba,  alisema, “natambua mengi yamesemwa baada ya tume, katika warsha na makongamano, na mjadala naomba mkumbuke hekima ya wahenga, yaliyopita si ndwele tugange yajayo. “
Alisema kila mwenye upande kwenye malumbano hayo, kama ingekuwa ni vita, angesema sasa mapigano yasimamishwe.
Tume ilitimiza wajibu wake, Bunge la Katiba limemaliza wajibu kilichobaki ni wananchi kupiga kura.  Pia alishukuru vyombo vya habari  akisema vimetoa mchango mkubwa wa mawazo kiasi cha mchakato kujulikana kwa wananchi.

No comments: