Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha), Halima
Mdee (35) na wenzake wanane wameachiwa kwa dhamana katika Mahakama ya Hakimu
Mkazi Kisutu.
Mdee na wanachama
wengine wanane waliachiwa jana mchana baada ya kutimiza masharti.
Masharti hayo yalikuwa kusaini hati ya dhamana ya Sh milioni
moja na kuwa na wadhamini wawili; mmoja awe mfanyakazi wa taasisi
inayofahamika, awasilishe barua ya muajiri na kutambulisho cha kazi.
Baada ya kuachiwa, Mdee ambaye pia ni Mbunge wa Kawe, alisema;
“walifikiri kunilaza Segerea siku moja wamenikomesha, nimekula bata ambayo
sijawahi kula, na walioamua kuficha barua za dhamana wajue kama tulikuwa
tunachechemea sasa tunakimbia”.
Mdee na wenzake walifikishwa mahakamani hapo juzi na
kusomewa mashitaka mawili ya kutotii amri halali ya Polisi na kufanya
mkusanyiko usio halali.
Walipelekwa rumande kwa kuwa upande wa Jamhuri ulikuwa
haujamaliza kukagua barua za wadhamini.
Washitakiwa hao wanadaiwa Oktoba 4, mwaka huu, katika mtaa
wa Ufipa, bila kuwa na uhalali hao walikiuka amri halali ya kutawanyika
iliyotolewa na Mrakibu wa Polisi (SP), Emmanuel Tillf kwa niaba ya Jeshi
la Polisi.
Katika mashitaka mengine, inadaiwa siku hiyo katika eneo
hilo, washitakiwa hao kwa pamoja, walifanya mkusanyiko usio halali kwa lengo la
kutembea kwenda kwenye Ofisi ya Rais. Walisomewa mashitaka mbele ya Hakimu
Mkazi, Janeth Kaluyenda.
Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Rose Moshi (45),
Renina Peter maarufu kama Lufyagila, Anna Linjewile (48), Mwanne Kassim (32),
Sophia F angel (28), Edward Julius (25), Martha Mtiko (27) na Beatu Mmari (35).
Upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na itatajwa tena Oktoba
21 kwa ajili ya usikilizwaji wa awali.
No comments:
Post a Comment