ASILIMIA 81 YA RASIMU YA WARIOBA YAMO KWENYE KATIBA PENDEKEZWA


Mwenyekiti wa Kamati ya Uandishi ya Bunge Maalumu la Katiba, Andrew Chenge amesema
asilimia 81.8 ya mapendekezo ya rasimu iliyowasilishwa bungeni na iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba yamo katika Katiba mpya Inayopendekezwa.
Chenge aliyasema hayo mjini hapa jana alipokuwa akitoa maelezo kuhusu uandishi wa
rasimu hiyo ya mwisho ya mapendekezo ya Katiba kwa Rais Jakaya Kikwete na Rais wa
Zanzibar, Dk Mohammed Shein.
Chenge aliyataja maeneo makubwa matatu ambayo rasimu ya mwisho ya Katiba
Inayopendekezwa imeyazingatia kuwa ni muundo wa Muungano, upungufu wa baadhi ya
mambo katika rasimu ya Tume na maboresho na marekebisho ya taaluma ya uandishi na
maneno katika baadhi ya ibara.
Akizungumzia Katiba mpya kuwa na mambo mengi yaliyopendekezwa na wananchi kupitia
iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Chenge alisema asilimia  81.8 ya maoni ya
wananchi kama walivyopendekeza kwenye Tume hiyo iliyokuwa chini ya Jaji Joseph
Warioba yamechukuliwa. Alisema Ibara 46 ambazo ni sawa na asilimia 10.7 zimefutwa na
Ibara 54 sawa na asilimia 18.2 ni mpya.
Kuhusu mabadiliko ya muundo wa serikali, Chenge alisema kutakuwa na Serikali mbili
na kwa mara ya kwanza sasa, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakuwa na Rais na
Makamu watatu wa Rais, ambao watatokana na mgombea mwenza atakayekuwa Makamu wa
Kwanza wa Rais, Rais wa Zanzibar atakuwa Makamu wa Pili wa Rais na Waziri Mkuu
atakuwa Makamu wa Tatu wa Rais.
Alisema pia Katiba hiyo Inayopendekezwa imeweka ukomo wa idadi ya mawaziri ambapo
sasa kutakuwa na Mawaziri na Naibu Mawaziri 40 tu, hatua itakayoipunguzia serikali
mzigo. Alisema Bunge pia litaundwa kwa kuzingatia uwiano na ukomo wa idadi ambapo
uwiano sasa utakuwa asilimia 50 kwa 50 kwa wanaume na wanawake na ukomo wa idadi
itakuwa wabunge kati ya 340 na 390.
Alisema ili kukidhi muundo huo mpya wa serikali ambao ulitofautiana na ule wa Tume
iliyopendekeza muundo wa serikali tatu, baadhi ya ibara ziliongezwa na nyingine
kufutwa, kuboreshwa au kubadilishwa ili kukidhi muundo mpya wa serikali na ibara
zilizoathirika zaidi ni  Ibara ya Kwanza na Sita ya Rasimu ya Tume.
Alisema kutokana na mabadiliko hayo, Rasimu ya Mwisho ya Katiba Inayopendekezwa
ambayo sasa itapelekwa kwa wananchi ili kupigiwa kura itakuwa na sura 19 zenye ibara
296 tofauti na ile ya Tume iliyokuwa na Sura 17 na Ibara 271.
"Mheshimiwa Rais, Bunge lilijadili rasimu ya Tume kupitia Kamati 12, ambapo mjadala
ulijielekeza katika kuboresha, kurekebisha, kupunguza na kuongeza ibara mpya kwa
kadri ilivyoonekana inafaa lakini rasimu ya Warioba ndio ilikuwa msingi wa mjadala,"
alisema Chenge.
Alisema Katiba inayopendekezwa imezingatia mambo muhimu mapya yakiwemo muundo  wa
serikali, utawala bora, haki za binadamu lakini pia uhuru kwa Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar kuanzisha uhusiano na taasisi yoyote ya kikanda au ya kimataifa kwa
masuala yanayoihusu Zanzibar.
Alisema mambo mengine mapya yaliyozingatiwa kwenye rasimu ya mwisho ya Katiba
Inayopendekezwa ni  suala la utafiti wa maendeleo, dira ya taifa ya maendeleo na
utekelezaji wa miradi ya maendeleo ya taifa, lengo likiwa ni kuhakikisha kuwa
rasilimali za nchi ikiwemo madini, mafuta na gesi zinalinufaisha taifa na Watanzania
kwa ujumla.
Kuhusu mambo yaliyotajwa na Tume kuwa ni Tunu za Taifa, Chenge alisema Bunge Maalum
la Katiba limeyaondoa mambo hayo ambayo ni uwazi, uwajibikaji, demokrasia, utawala
bora, utawala wa sheria, uzalendo, haki za binadamu na usawa wa kijinsia kutoka kuwa
tunu za taifa na kuwa misingi ya taifa.

No comments: