Wizara
ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi imewataka
wasimamizi wa mitihani ya darasa la saba unaotarajiwa kufanyika leo kufanya
kazi kwa umakini na kujiepusha na vitendo vya udanganyifu.
Hayo
yalisemwa jana na Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama
wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa na kueleza kuwa
maandalizi yote yamekamilika.
Alisema
Serikali itachukua hatua kali kwa msimamizi yeyote atakayegundulika kujihusisha
na udanganyifu wowote au kukiuka utaratibu katika kipindi chote cha usimamizi.
Kwa
mujibu wa Mhagama, watahiniwa 808,111 wanatarajia kufanya mtihani huo. Wavulana
ni 378,470 sawa na asilimia 46.84 na wasichana ni 429,641 sawa na asilimia
53.16. Watafanya jumla ya mitihani mitano Kiswahili, Kingereza, Sayansi,
Hisabati na Maarifa ya Jamii.
Aidha
alisema watahiniwa 783,223 watafanya mtihani kwa lugha ya Kiswahili na 24,888
watafanya kwa Kiingereza ambayo ndio lugha waliyokuwa wakitumia katika
kujifunzia katika elimu ya msingi.
Pia
alisema wapo watahiniwa 86 wasioona walioandikishwa kufanya mtihani, wavulana
ni 54 na wasichana ni 32 huku watahiniwa wenye uono hafifu ambao huhitaji
maandishi makubwa wapo 714, wavulana 371 na wasichana 343.
No comments:
Post a Comment