Zaidi ya
wanafunzi 96 wa kike wa Kidato cha Nne katika Shule ya Sekondari African Muslim
iliyopo mjini Moshi, wamenusurika kifo baada ya bweni walilokuwa wakilala,
kuteketea kwa moto usiku wa kuamkia jana mjini hapa.
Moto huo
ambao bado chanzo chake halisi hakijajulikana, ulianza saa 7:45 usiku, ulidumu
kwa zaidi ya saa tano, ukianzia katika choo cha shule hiyo jirani na Bweni la
Makka.
Baadaye moto
huo uliunguza chumba kinachofuata na
kusambaa kwenye vyumba 20 vilivyoko katika bweni hilo lenye ghorofa moja.
Mkurugenzi wa
Shule hiyo, Ali Adam Ali, alisema katika
tukio hilo wanafunzi wanne walipoteza fahamu kwa hofu na kukimbizwa hospitali
na sasa hali zao ni nzuri huku wanafunzi wengine wa Kidato cha Pili na Nne
wakijitahidi kuokoa baadhi ya mali zao.
Aidha
Mkurugenzi huyo alisema wanafunzi hao walikuwa hawajaingia kulala na wakati huo
walikuwa wakijiandaa kwa sala ya Isha ambapo mmoja wa wanafunzi aliwajulisha
wenzake juu ya kuhisi harufu kali ya moshi na baadaye kutoa taarifa za kuwapo
kwa moto huo.
Ali alisema
moto huo umesababisha hasara ya mamilioni ya shilingi kwani wanafunzi hao
walipoteza baadhi ya vitu vyao ikiwamo vitabu, vitanda na nguo.
Ulizimwa na
Kikosi cha Zimamoto na Uokoaji cha Manispaa ya Moshi.
Miongoni mwa
viongozi waliofika shuleni hapo ni pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya
Mkoa, ikiongozwa na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Dk Ibrahim Msengi.
Msengi
aliagiza uongozi wa shule hiyo kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi wa Manispaa
kufanya tathimni ya hasara iliyopatikana.
Aidha katika
agizo hilo, Dk Msengi alimtaka Mkurugenzi wa shule kufuatilia kwa makini chanzo
cha moto huo na kuwasilisha taarifa mezani kwake mapema iwezekanavyo.
Wakati huo
huo, Kaimu Ofisa Elimu Mkoa wa Kilimanjaro, Estomih Makyara amemtaka Mkurugenzi
wa shule hiyo kutoa wiki moja ya mapumziko kwa wanafunzi walioathirika na moto
huo.
No comments:
Post a Comment