WAFA KATIKA AJALI WAKITOKA KUZIKA MWENZAO MUSOMA


Watu wawili wamekufa na wengine watano kujeruhiwa baada ya magari mawili, likiwamo basi dogo la abiria walilokuwa wakisafiria kugongana uso kwa uso na lori la mafuta.
Kwa mujibu wa Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, Athuman Mwambalaswa alisema kuwa tukio hilo lilihusisha gari aina ya Toyota Coaster lililokuwa linatokea kwenye msiba Musoma mkoani Mara kwenda Dar es Salaam na kugongana na lori la mafuta.
Kamanda Mwambalaswa alisema kuwa ajali hiyo ilitokea juzi maeneo ya Ubena Senge katika barabara ya Morogoro, chanzo kikitajwa kuwa ni uzembe wa gari dogo aliyehama upande wake kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni uchovu wa safari ndefu.
Alisema basi dogo lenye namba za usajili namba T 663 BKP lililokuwa likiendeshwa na Ally Abdul (34), likiwa na abiria 20 liligongana na lori la mafuta aina ya Leyland Daf lenye namba za usajili T 858 CLK na tela namba T 421 CKY, mali ya kampuni ya Ramader ya Dar es Salaam ambalo dereva wake ametajwa kwa jina moja la Rashid.
Aliwataja waliokufa kwenye ajali hiyo kuwa ni Neema Mile (39) na Jane Mtani (38) ambao miili yao imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Pwani, Tumbi ambako pia majeruhi wamelazwa.

No comments: