WABUNGE WAPENDEKEZA WALARUSHWA WANYONGWE



Baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wamesema wala rushwa pamoja na wahujumu uchumi adhabu yao iwe ni kunyongwa.
Wametaka  Katiba mpya inayoenda kuandikwa itamke hivyo ili kufanya viongozi wa kisiasa kuogopa kama ilivyo kwenye nchi nyingine.
Sababu ya wajumbe hao kupendekeza jambo hilo ni kwamba uhujumu uchumi na rushwa nchini limekuwa tatizo kubwa  kwa viongozi.
Kutokana na ukiukwaji huo wa maadili, wamesema  umefika wakati wa kuweka bayana suala hilo kwenye sheria mama.
Miongoni mwa waliochangia ni Paul  Makonda aliyesema suala hilo likiwekwa bayana, litaokoa fedha nyingi za walipa kodi ambazo kwa sasa baadhi ya viongozi wanazichota na kwenda kuzihifadhi nje ya nchi.
Pia alipinga kuruhusu viongozi wa nchi kufungua akaunti nje ya nchi. “Kwa nini viongozi hao washindwe kuhifadhi fedha zao ndani ya nchi, wanafanya biashara gani hadi wakafungue benki nje ya nchi?
“Tusiruhusu jambo hili na napendekeza kwamba kiongozi atakayebainika amekula rushwa na kuhujumu uchumi huyo anyongwe,” alisema Makonda.
Yusuf Singo pia alisema maadili yanazidi kuporomoka kwa viongozi,  jambo linalorudisha nchi nyuma. Alitaka Katiba isisitize maadili kwa kada hiyo na ambao watakiuka wanyongwe.
Alitoa mfano wa Japan kuwa kiongozi wa kisiasa anapochunguzwa kwa kujihusisha na rushwa anatoa machozi kwa sababu hajui hatima yake. “Tunataka na sisi ifike wakati kiongozi akianza kuchunguzwa atoe machozi,” alisema.
Dk Mary Mwanjelwa katika mchango wake alisema rushwa imekuwa adui mkubwa wa maendeleo ya Watanzania. Alisema isipopingwa kuanzia kwenye Katiba, nchi itakuwa inajichora.
Alisema Bunge halitaeleweka kama halitaweka jambo hilo kwenye Katiba, kwa sababu wananchi wengi wameteseka ndani ya nchi yao kwa sababu ya rushwa.
Alisema pia wapo viongozi wengi wasio na maadili  na ndiyo maana wanajihusisha na vitendo vya rushwa.
Kwa upande wake, Profesa Mark Mwandosya alisema tatizo la rushwa haliwezi kutenganishwa na haki za binadamu kutokana na kukosesha wananchi maendeleo.
Profesa Mwandosya alisema Katiba lazima itambue adui wa haki za wananchi ni rushwa.
Alipendekeza suala hilo litambulike kikatiba na serikali zote mbili zitunge sheria kali za kupambana na rushwa  kuhakikisha wananchi wanapata haki zao za msingi bila kutoa wala kupokea rushwa.
Naye Gerison Lwenge  alisema Katiba itambue jambo hilo na ikemee vikali kwa wanaotoa na wale wanaopokea.
Alisema kwa ahli ilivyo, wanaobanwa zaidi ni wale ambao wanapokea na akapendekeza sheria kali zitungwe kubana pia wanaotoa.
Alishauri Kamisheni isimamie suala hilo la rushwa badala ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Kwa mujibu wa Lwenge, Kamisheni ni chombo kikubwa zaidi kuliko ilivyo kwa taasisi. Alisema kazi yake itakuwa ni kuzuia zaidi na si  kutibu pekee.
Jesca Msambatavangu alisema Takukuru wanafanya kazi vizuri na walishindwa kupambana na rushwa kwa vile hawana uhuru wa kutosha.
Alisema kama Takukuru wakipewa meno kupitia Katiba mpya, watashughulika kwa uhuru zaidi katika kupambana na tatizo la rushwa nchini.

No comments: