Wanafunzi wa
darasa la saba mkoani hapa wamefanya mitihani yao ya kuhitimu elimu hiyo kwa
utulivu na usalama mkubwa kutokana na kuwepo kwa maandalizi ya kutosha.
Ofisa Elimu
wa Mkoa, Raymond Mapunda alisema hayo jana wakati akizungumza na HabariLeo na
kuongeza kuwa mtihani huo umefanyika katika shule 511 katika hali ya amani na
utulivu huku kukiwa na ulinzi katika maeneo yote.
Alisema
wanafunzi 60,710 ndio walioandikishwa kwa ajili ya kufanya mtihani huo na kila
chumba cha mtihani chenye wanafunzi 25 kitakuwa na msimamizi mmoja.
“Tunategemea
mtihani kumalizika kwa amani bila kuwepo kwa udanganyifu wowote… kwani
maandalizi yalikuwa mazuri na ya kutosha yakitegemewa kuwa na ufaulu mkubwa,”
alisema Mapunda.
Kuhusu
usimamizi katika chumba cha mtihani alisema ni walimu waliopewa mafunzo maalumu
na kwamba hawatoki katika shule wanazozisimamia.
Mapunda
alisema kwa siku ya jana wanafunzi hao walifanya mitihani ya Hisabati, Sayansi na Kiswahili.
Kuhusu
mategemeo ya Mkoa alisema wanatarajia kuwepo kwa matokeo mazuri kutokana na
kwamba tangu mwaka ulipoanza hapajakuwepo kwa migomo au migogoro ya walimu
ambayo ingesababisha kuonekana kama ufundishaji haukukidhi matakwa stahiki.
Kuhusu vifaa
katika vyumba vya mitihani alisema hali ni shwari na hadi wanafunzi hao
wanafanya mtihani wao wa tatu, ofisi yake haikupata malalamiko yoyote yenye
kuhusiana na upungufu.
Akizungumzia
mtihani huo juzi, Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama
alisema watahiniwa 808,111 wanatarajiwa kufanya mtihani huo.
Wavulana ni
378,470 sawa na asilimia 46.84 na wasichana ni 429,641 sawa na asilimia 53.16
ambao watafanya mitihani mitano ya Kiswahili, Kiingereza, Sayansi, Hisabati na
Maarifa ya jamii.
No comments:
Post a Comment