UTALII WACHANGIA SHILINGI TRILIONI 3 KWENYE PATO LA TAIFA


Sekta ya Utalii nchini imekuwa ikichangia pato la Taifa kwa kiasi kikubwa, ambapo kwa mwaka jana ilichangia dola bilioni 1.8 (Sh trilioni 3) katika pato hilo.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), Devota Mdachi alisema hayo jijini Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Onesho la Kimataifa la Utalii (SITE).
Alisema sekta hiyo imekuwa na mchango mkubwa. Alisema kutokana na ukuaji wake, wameamua kuanzisha onesho hilo, ambalo litakuwa likifanyika kila mwaka.
“Kwa mwaka huu maonesho hilo kubwa la kimataifa litafanyika kuanzia Oktoba mosi hadi nne ambapo watakuwepo wageni kutoka nchi mbalimbali kwa lengo la kutangaza utalii,” alisema.
Alisema katika kufanikisha maonesho hayo, wamewashirikisha wadau mbalimbali, wakiwemo TANAPA, Hifadhi ya Ngorongoro, Kampuni ya ndege ya Ethiopia, makampuni na mashirika mengine, ambapo TTB imechangia Sh milioni 500 katika maandalizi hayo.
Alitoa mwito kwa watanzania kujitokeza kwa wingi katika maonesho hayo ili kujifunza utalii wa ndani na kujivunia vivutio vilivyopo na kutafuta soko kupitia wadau  walioalikwa katika maonesho hayo.
Mratibu Mkuu wa maonesho hayo, Philip Chitaunga alisema lengo la maonesho hayo ni kuwakutanisha watanzania na masoko ya nje na pia watawaleta wadau mbalimbali wanaoandika habari za utalii na wadau wenye makampuni ya watalii.
Wageni hao pia watapata fursa ya kufanya ziara kwenye vivutio mbalimbali, ikiwemo Zanzibar na Ngorongoro, ambapo kwa watanzania itakuwa ni fursa kwa wenye makampuni ya watalii kujitangaza na kutafuta soko.

No comments: