PINGAMIZI LA MWANASHERIA MKUU DHIDI YA TLS LATUPILIWA MBALI

Pingamizi la Mwanasheria Mkuu (AG) dhidi ya ombi la kibali cha kufungua kesi ya kupinga vikao vya Bunge Maalumu la Katiba vinavyoendelea mkoani Dodoma limetupiliwa mbali katika
Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam. Pingamizi hilo lilikuwa la kupinga ombi lililowasilishwa na Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS) waliofungua kesi ya kikatiba wakiomba mahakama itoe zuio la kuendelea kwa vikao vya Bunge maalumu la katiba hadi kesi hiyo itakapokwisha.
Aidha, wanaomba Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) awasilishe bungeni muswada wa marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba namba 8 ya mwaka 2011 na namba 2 ya
mwaka 2012, sura ya 83 na ifafanue kifungu cha 25 cha sheria hiyo. 
 Uamuzi huo ulitolewa jana na jopo la majaji watatu wanaosikiliza ombi hilo wakiongozwa na Jaji Augustine Mwarija, Dk Fauz Twaib na Aloyisius Mujulizi.
Wakati huo huo, kesi nyingine ya kikatiba iliyofunguliwa na Mwandishi wa Habari, Saidi Kubenea akihoji mamlaka ya Bunge hilo inaanza kusikilizwa leo ambapo ilitakiwa ianze kusikilizwa jana lakini AG aliwasilisha pingamizi ambalo pia litaendelea kusikilizwa leo.
Katika kesi hiyo, Kubenea anaiomba mahakama hiyo itoe tafsiri sahihi ya Mamlaka ya Bunge la Katiba, kwa kuzingatia kifungu cha 25 (1) na (2) cha Sheria ya Mbadiliko ya Katiba namba 83 ya mwaka 2011.
Aidha, anaiomba mahakama itamke kama bunge hilo lina mamlaka ya kubadilisha maudhui ya Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kwa kiwango gani.

No comments: