Kivuko
cha Mv Kigamboni kilichokuwa kwenye matengenezo, kinatarajiwa kuanza kutoa
huduma kesho na Serikali imeokoa zaidi ya Sh milioni 300 kwa kufanya
matengenezo hayo hapa nchini.
Sambamba
na hilo, Serikali imesema kivuko kipya cha Dar es Salaam kwenda Bagamoyo
kinatarajiwa kuingia nchini baada ya wiki nne na kitasaidia kupunguza foleni ya
Jiji la Dar es Salaam. Kivuko hicho kilitengenezwa kwa ushirikiano na Serikali
ya Denmark kwa gharama ya Sh bilioni 7.9.
Hayo
yalisemwa jana jijini Dar es Salaam na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli
alipotembelea eneo kinapofanyiwa matengenezo na Jeshi la Wananchi wa Tanzania
(JWTZ) Kamandi ya Maji.
Alisema
matengenezo yaliyofanywa na jeshi hilo, yameokoa zaidi ya nusu ya fedha
iliyokuwa imekadiriwa kukarabati kivuko hicho Mombasa nchini Kenya, ambapo
makadirio yake yalikuwa zaidi ya Sh milioni 600.
“Natoa pongezi kwa kazi nzuri inayofanywa na
JWTZ ukiwemo ukarabati wa kivuko hiki, ni kweli kivuko tungekipeleka nje
gharama ya matengenezo ingekuwa kubwa kuliko ilivyo sasa na pia tusingekuwa na
uhakika kama wananchi wangeweza kukitumia wiki hii kwa kuwa kingechukua muda
mrefu ila nyie mmefanya kazi kwa moyo wa kizalendo,” alisema.
Alisema
kazi waliyoifanya wanajeshi hao ni kubwa na kutoa mwito kwa taasisi nyingine,
kutokimbilia watu wa nje kufanya kazi zao, badala yake watoe fursa kwa
Watanzania kwanza kwa kuwa nao wanaweza.
“Nawaahidi
kivuko cha Mv Kigamboni kikirudi mjipange tena kwa sababu tutawaletea Kivuko
cha Mv Magogoni nacho mkifanyie matengenezo kwa kuwa muda wake umewadia. Nataka
hata kama kuna kushindanishwa nyie ndiyo mshinde kwa kuwa mmefanya kazi nzuri
na pia nyie siyo wezi,” alisema.
Alisema
“kama kivuko hicho kingetengenezwa huko nje usalama na ubora wake ungekuwa wa
mashaka kwa sababu hata tusingepata muda wa kuja kukitembelea na kukagua kazi
inavyoendelea kama tunavyofanya sasa na hata tungetuma watu pengine nao wangeongea nao vizuri”.
Aliwaomba
wanajeshi hao kuingiza kivuko hicho kwenye maji leo jioni ili wananchi wa
Kigamboni wakitumie kesho kwa sababu kazi kubwa imemalizika na kilichobaki ni
kumalizia mambo madogo ikiwemo kupaka
rangi.
Alisema
Wizara yake itaendelea kutumia utaalamu wa jeshi hilo katika kazi zake na
kutokana na kuridhishwa na kazi nzuri,
Dk Magufuli alitoa ng’ombe wawili kwa ajili ya mafundi hao kusherehekea
kazi waliyoifanya.
Kuhusu
kivuko kipya cha Dar es Salaam kwenda Bagamoyo, alisema kinatarajiwa kuingia nchini
kutoka Denmark baada ya wiki chache.
“Tuliahidi
kuwa kitakuja kivuko kipya cha Dar es Salaam kwenda Bagamoyo kupunguza
msongamano, leo hii kimeingia majini huko na baada ya wiki tatu hadi nne
kitakuwa kimeshafika nchini,” alisema Magufuli.
Awali,
Mkuu wa Kamandi hiyo, Brigedia Jenerali Rogastian Laswai alisema mafundi
walioshiriki katika matengenezo hayo ni 55, wakiwemo wahandisi, mafundi mchundo
na vibarua.
No comments:
Post a Comment