Mtuhumiwa
katika kesi ya ugaidi, Abdallah Maginga, ameiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi
Arusha, kumruhusu kutohudhuria siku za kesi na abaki magereza, kutokana na
maumivu makali anayodai anayapata sehemu za siri alikominywa na polisi na
kuingiziwa mti kwenye haja kubwa.
“Mheshimiwa
Hakimu naomba mahakama yako inipe ruhusa ya kutohudhuria siku ya kesi, sababu
ninapopanda gari napata maumivu makali sana sehemu za siri kunauma kwa sababu
polisi walinitesa kwa kuniingizia mti kwenye haja kubwa na kuminya sehemu zangu
za siri,” alisema.
Alisema
mbele ya Wakili wa Serikali, Rose Sulle kuwa mbali na maumivu ya sehemu za
siri, pia mguu wake uliokatwa hospitalini, bado unamsumbua kutokana na maumivu.
Maginga
pia aliomba iagize Magereza wamruhusu akatibiwe hospitalini, kwani alitakiwa
kwenda kupata matibabu Septemba 5 mwaka huu, ila alizuiwa hadi sasa.
Akijibu
hoja hizo, Hakimu aliyesikiliza kesi hiyo, Devotha Msofe, alisema suala la kuja mahakamani ni lazima na
mahakama haiwezi kumpa ruhusa hiyo.
Pia,
alimshauri mshitakiwa huyo kuwa kama ana maelezo mengi, amweleze hakimu
anayesikiliza kesi yake, Mustapher Siyani ambaye kwa siku hiyo hakuwepo.
“Sikiliza
Maginga suala la kuja mahakamani ni lazima na sio hiyari wala majadiliano, ila
kuhusu kwenda hospitalini liwasilishe Magereza ndio mtaona kwa pamoja
mnafanyaje,” alisema.
Awali
ilidaiwa mahakamani hapo kuwa washitakiwa
hao wameshitakiwa kwa makosa yaliyo chini ya Sheria ya Kuzuia ugaidi,
ambapo Sheria Namba 22 ya Mwaka 2002
inasema upelelezi ukishakamilika, Mahakama Kuu ndiyo yenye mamlaka ya
kuisikiliza na kutoa uamuzi.
Washitakiwa
hao wanakabiliwa na mashitaka ya kuua, kujaribu kuua, kusajili na kusafirisha
vijana kujiunga na Al-Shabaab.
Mbali
na mashitaka hayo, pia wanahusishwa na
tukio la mlipuko wa bomu
lilitokea baa ya Arusha Night Park
jijini Arusha na kusababisha kifo cha mtu mmoja na kujeruhi wengine 16.
Watuhumiwa wengine wanaokabiliwa na
mashitaka hayo ni Abdallah Athumani, Abdallah Thabiti, Ally Hamisi, Abdallah
Wambura, Rajab Hemedi, Hassan Saidi, Ally Hamisi, Yassin Sanga, Shaaban Wawa,
Swaleh Hamisi, Abdallah Yassin, Abdallah Maginga na Sudi Nassib Lusuma. Wengine
walioongezwa katika shauri hilo ni Shaaban Mussa, Athuman Hussein, Mohammed
Nuru, Jafari Lema, Abdul Mohammed na Said Michael Temba.
No comments:
Post a Comment