MSAKO WA BODABODA ZENYE NAMBA ZA NJANO WAANZA



Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) imesema usajili wa pikipiki maarufu kama ‘bodaboda’ utafanywa pamoja na kukagua namba zenye rangi ya njano huku zikiwa zinafanya biashara, jambo ambalo ni kinyume.
Meneja Mawasiliano wa Sumatra, David  Mziray alisema hayo Dar es Salaam wakati akizungumza na  HabariLeo kuhusu usajili wa namba za pikipiki pamoja na zenye magurudumu matatu ili ufanywe pamoja na kukagua rangi zinazotakiwa kwa biashara.
Usajili wa namba za pikipiki na zenye magurudumu matatu unatarajiwa kufanywa na Mamlaka ya Mapato nchini (TRA) ambapo namba zote zitabadilishwa kuanzia Oktoba mosi.
Akizungumzia usajili huo, Mziray alisema kimsingi kazi hiyo itafanywa na TRA lakini Mamlaka hiyo inaiomba Mamlaka ya Mapato kuendesha usajili pamoja na ukaguzi wa rangi za namba za pikipiki.
“Zipo bodaboda nyingi ambazo zina rangi za njano na ambazo zinaendelea kutoa huduma kibiashara wakati rangi inayotakiwa ni  nyeupe…tumewaambia TRA wakati wa usajili huo wakague pia,” alisema Mziray.
Alisema wamiliki wengi wa pikipiki wanapoagiza vifaa hivyo wakati wa kuvitoa bandarini hudanganya kana kwamba sio vya biashara ili kukwepa kulipa kodi lakini baadae huonekana mitaani vikifanya kazi kibiashara.
Alisema kutokana na usajili huo kufanywa na TRA, Mamlaka ya Sumatra itafanya ukaguzi huo ili kupunguza mianya ya wasiolipa kodi.
Kuhusu usajili huo, taarifa ya Idara ya Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi ilifafanua kuwa TRA inawataka wamiliki wote wa vifaa hivyo kuwa mfumo mpya wa usajili wa namba za pikipiki unaoanzia namba MC 101 AAA badala ya namba zinazotumika sasa.
“Kwa mantiki hiyo wamiliki wote namba zote zitabadilishwa kuanzia Oktoba mosi, hivyo wafike katika ofisi za TRA kwa ajili ya kazi hiyo,” alieleza taarifa hiyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kazi ya ubadilishaji wa namba hizo utafanywa bila adhabu kwa kipindi cha miezi sita kuanzia Oktoba mosi mpaka Machi 31, mwakani na baada ya muda huo ubadilishwaji utafanywa na adhabu.

No comments: