Mchakato
wa kuandika Katiba mpya kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao umekwama, baada ya viongozi
wa vyama vya siasa vyenye wabunge na Rais Jakaya Kikwete, kukubaliana
kusitisha mchakato huo.
Badala
yake viongozi hao wa vyama vya siasa wamekubaliana kwamba Katiba ya sasa ya
mwaka 1977, ipelekwe bungeni kufanyiwa marekebisho, ili kutoa fursa Uchaguzi
Mkuu ujao ufanyike mwakani kisha mchakato wa Katiba mpya, uendelee baada ya
uchaguzi huo.
Mambo
ambayo vyama vya siasa wamekubaliana, ni kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi
itakayosimamia uchaguzi wa mwaka 2015; mshindi wa uchaguzi wa Rais apate zaidi
ya asilimia 50 ya kura zote, matokeo ya uchaguzi wa rais yaruhusiwe kupingwa
mahakamani na kuruhusu mgombea binafsi katika uchaguzi.
Pia
vyama vingine vya siasa ambavyo vinataka kupendekeza mambo mengine ya
kurekebisha katika Katiba ya mwaka 1977, vimeombwa kufanya hivyo mapema kwa
kuwa muda uliopo wa kufanya mabadiliko ni mdogo.
Kutokana
na mabadiliko hayo, TCD kupitia vikao vyake, itaratibu na kujadili mapendekezo
hayo na kupeleka serikalini kwa hatua zingine za kuingiza mapendekezo hayo
kwenye marekebisho ya Katiba.
“Muda
tulio nao ni kwa mabadiliko yanayopendekezwa kujadiliwa katika Bunge la
Novemba na wakichelewa Bunge la Februari 2015," alisema John Cheyo wakati
akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa.
Kwa
makubaliano hayo, kazi inayofanywa na Bunge Maalumu la Katiba (BMK) ya
kuandika Katiba mpya itakoma Oktoba 4 mwaka huu, siku ambayo Bunge hilo
litakuwa halijakamilisha uandikaji wa Katiba, ambao unafanywa na kamati ya
uandishi iliyo chini ya Andrew Chenge.
Alipoulizwa
kama Rais atakayekuja asipoona Katiba kama kipaumbele itakuwaje, Cheyo alisema
yeye na viongozi wenzake wanaamini kuwa kiongozi huyo atashauriana na wenzake
ili kukamilisha mchakato huo.
"Rais
ana uhuru wake, tusimwekee masharti Rais ajaye," alisema Cheyo. Hata hivyo
hakuweka bayana kama mchato huo utaanzia pale ulipomalizikia au utaanza upya.
Uamuzi
huo unakidhi baadhi ya madai ya kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa)
ambao ni wajumbe waliokuwa ndani ya Bunge Maalumu la Katiba, lakini walijiondoa
kwa madai ya kutoridhishwa na mwenendo wa Bunge hilo.
Kutokana
na msimamo wao wa kutorejea bungeni hata baada ya kuombwa kufanya hivyo na
viongozi mbalimbali, kundi hilo lilitia ngumu badala yake wakataka kukutana na
Rais Kikwete.
Miongoni
mwa madai yao waliyokuwa wanayataka ya kusitisha Bunge hilo hayakufanikiwa kwani
litaenda hadi mwisho kwa kuwa lipo kisheria.
Ratiba
ya Bunge inaonesha kuwa majadiliano ya wabunge ambayo yalianza jana,
yangekuchukua siku 15 na yangekamilika Septemba 29. Septemba 30 hadi Oktoba 6
Kamati ya Uandishi ilitengewa siku tano kwa ajili ya kuandika Katiba
inayopendekezwa na Bunge Maalumu.
Oktoba
9 Kamati ya Uandishi ilikuwa iwasilishe Katiba hiyo bungeni na Oktoba 10 hadi
Oktoba 21 ingekuwa siku saba kwa ajili ya kupiga kura. Baada ya hapo Bunge
lilijipangia kuwa baada ya upigaji kura, wajumbe wangepewa siku tano kwa ajili
ya kujadili na kupitisha masharti ya mpito.
Ratiba
hiyo ya Bunge pia inaonesha kuwa Oktoba 29 na 30, Mwenyekiti wa Bunge Maalumu
alikuwa awasilishe kwa Rais Katiba inayopendekezwa na Bunge lake.
Mwenyekiti
wa Kituo cha Demokrasia (TCD) Cheyo alitaja sababu saba zilizowaongoza
kuafikiana mambo hayo; moja ni Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, inayotaka mwisho
wa mchakato wa kupata Katiba mpya, uwe kura ya maoni iliyotarajiwa kufanyika Aprili 2015.
Cheyo
alisema kama itabidi kura kurudiwa kwa mujibu wa sheria iliyotajwa, ilitarajiwa
kufanyika hivyo Julai 2015, muda ambao Bunge la Muungano linatakiwa liwe
limevunjwa kwa ajili ya kupisha Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2015.
Alisema
ili Katiba mpya itumike katika uchaguzi mkuu utakaokuja, ilionekana kuwa
itabidi uhai wa Bunge na Serikali uongezwe zaidi ya 2015, jambo ambalo alisema
viongozi wa vyama vya siasa hawaliungi mkono jambo hilo.
Alitaja
sababu ya pili ni kwamba Bunge Maalumu la Katiba kwa sasa linafanya kazi
kwa mujibu wa tangazo la Serikali namba 254 lililotolewa na Rais Kikwete Agosti
mosi mwaka huu. Tangazo hilo litatumika hadi Oktoba 4, mwaka huu ambapo Katiba
inayopendekezwa ilitarajiwa kupatikana.
Alisema
wajumbe walikubaliana hatua hiyo iachwe iendelee hadi ifikie mwisho, kama
tangazo linavyoelekeza kuwa mwisho itakuwa Oktoba 4.
Cheyo
alisema pia kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, baada ya Bunge
Maalumu la Katiba kumaliza kutunga Katiba, ingefuata hatua ya kura ya maoni
kuthibitisha Katiba.
Alisema
kwa kutambua kuwa hatua ya kura ya maoni italazimisha Uchaguzi Mkuu 2015
kuahirishwa hivyo hatua hiyo lazima iahirishwe.
Cheyo
alisema sababu nyingine ni mchakato wa Katiba uendelee baada ya Uchaguzi Mkuu
wa 2015.
Hivyo
viongozi hao wamekubaliana Katiba ya sasa ifanyiwe marekebisho haraka, ili
kusaidia kufanyika kwa uchaguzi wa serikali za mitaa haraka iwezekanavyo.
Katika eneo hilo viongozi hao wametaka Serikali kuchukua hatua za kisheria, ili
uchaguzi huo ufanyike mapema mwakani.
Vyama
vilivyoshiriki kwenye mazungumzo hayo ni Chama Cha Mapinduzi (CCM), Chama cha
Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Chama cha Wananchi (CUF) NCCR Mageuzi,
Tanzania Labour Party (TLP), United Democratic Party (UDP) na chama cha United
Peoples Democratic Party (UPDP).
No comments:
Post a Comment