MACHINGA WAJIHALALISHIA UWEPO WAO KATIKATI YA JIJI


Wafanyabiashara ndogo (wamachinga) wamedai hatua ya kuondolewa katika maeneo mbalimbali ya jiji  wasifanye biashara, huenda ikachukua muda mrefu kufanikiwa, kwa kile walichodai wana ‘mikataba’ maalumu na mgambo  wa jiji.
Baadhi ya wafanyabiashara hao, walisema ni vigumu kuwaondoa kwani wana makubaliano maalumu ya malipo ya kila siku kati yao na mgambo na utaratibu wa kufanya biashara, hatua inayowawezesha kuendesha maisha yao.
Mmoja wa wafanyabiashara hao aliyejitaja kwa jina la Hussein, aliyekuwa akifanya biashara kituo cha daladala cha Mwenge kabla hakijahamishwa, alisema kabla ya kuondoka eneo hilo, kila siku yeye na wenzake walilazimika kutoa fedha kwa mgambo ili kupata ridhaa ya kufanya biashara katika eneo hilo.
“Unajua pale hakukuwepo na utaratibu maalumu wa biashara hasa kwa sisi tuliokuwa tumeweka meza zetu pembezoni hivyo tulilazimika kulipa hela kila siku, malipo yalitegemea unaweza ukatoa Shilingi 3,000 hadi Shilingi 7,000 kwa siku hiyo ni kwa kila mtu,” alisema Hussein.
Pia mfanyabiashara mwingine wa Ubungo Darajani, ambaye hata hivyo hakuwa tayari kutaja jina lake, alisema eneo la Manzese anapofanya shughuli zake mchana kabla ya kuhamia darajani jioni, analazimika kutoa hela aweze kufanya shughuli zake.
Ofisa Habari wa Manispaa ya Kinondoni, Sebastian Mhowera, alipotafutwa kuzungumzia hilo hakupatikana baada ya simu yake ya mkononi kutopokewa. Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki akiahidi kulishughulikia suala hilo.
“Tutalifanyia kazi suala hili kwa kawaida mnapokuwa wengi katika jambo moja wapo watakaozunguka na kuwakwamisha, hii hali kwa vyovyote ndiyo inayokwamisha mpango wetu wa kuliboresha jiji hili” alisema Sadiki.

No comments: