Jeshi la Polisi nchini limepiga marufuku
maandamano ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), yaliyotarajiwa
kuanza kufanyika leo katika maeneo mbalimbali nchini.
Jeshi
hilo limeonya kuwa maandamano hayo ni batili na ni kinyume cha sheria.
Akizungumza
na waandishi wa habari jana makao makuu ya jeshi la Polisi Dar es Salaam,
Kamishna wa Polisi wa Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja alisema jeshi hilo
limeanza kupokea taarifa ya chama hicho, kikitaka kufanya maandamano kuanzia
leo. Lakini, alisisitiza kuwa maandamano hayo hayataruhusiwa.
“Septemba
15 jeshi lilitoa taarifa kuhusu kauli iliyotolewa na Mwenyekiti wa Chadema,
Freeman Mbowe akiwahimiza wafuasi wa chama chake kufanya maandamano na migomo
isiyokoma pote nchini ili kusitishwa kwa Bunge la Katiba na hivi sasa tumeanza
kupokea taarifa ya chama hicho kufanya maandamano,” alisema.
Alisema
maandamano hayo ni batili, kwa sababu Bunge la Katiba linaloendelea hivi sasa,
linafanyika kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na hakuna sheria
iliyokiukwa, hivyo kitendo cha kufanya maandamano, kushinikiza kuvunjwa kwa
Bunge hilo ni kinyume cha sheria, jambo ambalo jeshi la polisi haliwezi
kuruhusu.
Aidha,
alisema kuwa ieleweke wazi kwamba Bunge la Katiba, lipo kisheria na kila jambo
linalofanyika bungeni ni kwa mujibu wa sheria.
Chagonja
alisema jeshi la polisi lina jukumu la kulinda watu wote, wanaotekeleza
majukumu yao kwa mujibu wa sheria.
“Hata
hivyo, hivi sasa kuna kesi inayoendelea Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam,
inayohoji uhalali wa kuendelea kwa Bunge hilo na kesi hiyo haijafikia mwisho na
uamuzi kutolewa, hivyo maandamano hayo yaliyopangwa na Chadema yanaingilia
uhuru wa Mahakama, jambo ambalo siyo sahihi. Mahakama kama chombo cha kutoa
haki, kiachwe kifanye kazi yake,”
alisema.
Chagonja
alitoa mwito kwa wananchi wote, kuendelea na shughuli zao na yeyote
atakayekiuka katazo hilo, jeshi la polisi halitasita kumchukulia hatua kali kwa
mujibu wa sheria.
Wakati
Chagonja akiyasema hayo, Kamanda wa Polisi mkoani Dodoma, amewaonya wafuasi wa
Chadema wanaodaiwa kutaka kuandamana hadi Viwanja vya Bunge
kushinikiza
kusitishwa kwa Bunge Maalumu la Katiba.
Hata
hivyo, uongozi wa Chadema mkoani humo, umedaiwa kusisitiza maandamano yako
palepale.
Akizungumza
jana, Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Emmanuel Lukula alisema
maandamano hayo, pia yamepangwa kufanyika katika wilaya zote za mkoa wa Dodoma.
Alisema
juzi walipokea taarifa kutoka kwa Uongozi wa Chadema Mkoa wa Dodoma, juu ya
kufanya maandamano ya amani kuanzia viwanja vya Nyerere Square hadi viwanja vya
Bunge kuanzia saa 4 asubuhi hadi saa 6 mchana.
Alisema
taarifa ya maandamano kama hayo, yanayotarajia kufanyika katika wilaya zote za
mkoa wa Dodoma, ilitolewa jana ambapo ni muda ulio kinyume na sheria ya kutoa
taarifa za maandamano ndani ya saa 48.
Alisema
katika barua ya chama hicho kwenda kwa Jeshi la Polisi, viongozi wa Chadema wa Mkoa huo, walisema wanapinga Bunge la
Katiba na wanataka kupaza sauti zao,
zisikike dunia nzima na walisisitiza kufanya maandamano hayo leo.
“Walikuja
hapa viongozi wa Chadema Mkoa, tulikaa nao kwenye mazungumzo zaidi ya saa
mbili, tuliwaambia Bunge lipo kwa mujibu wa sheria za nchi na hakuna mahakama
iliyotamka Bunge lisitishwe, lakini walisisitiza kuwa maandamano yako pale
pale,” alisema.
“Maandamano
hayo ni batili yanapinga chombo ambacho kipo kwa mujibu wa sheria, tunasisitiza
wananchi wa Dodoma wasishiriki maandamano hayo, hayana tija hata kidogo na
wananchi wasijitokeze waendelee na shughuli zao,” alisema.
Alisema
maandamano ni haki ya kikatiba, lakini wanatakiwa kufuata sheria. Alisema Jeshi
la Polisi limejipanga kudhibiti maandamano hayo katika wilaya zote, kutokana na
viongozi wa Chadema kukaidi amri ya kutaka kusitisha maandamano hayo.
Wakati
jeshi la Polisi likichukua hatua hiyo, Umoja wa Vijana Wazalendo wa Vyuo vya
Elimu ya Juu Dar es Salaam, nao umejitokeza na kulaani kauli zilizotolewa na
Mbowe za kuhamasisha maandamano na migomo nchi nzima, hata kama jeshi la Polisi
halitabariki kufanyika kwa mambo hayo.
Mwenyekiti
wa Umoja huo, Mussa Omar anayesoma Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT), alisema
umoja huo ni Muungano wa vyuo 14 vya elimu
ya juu vilivyopo Dar es Salaam.
Alisema
Watanzania wengi wamekerwa na kusononeshwa na kauli ya kiongozi huyo ya
kuhamasisha maandamano, alizozitoa wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa
uchaguzi wa Chadema, mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam.
“Tumemsikia
akiahidi maandamano bila kikomo kwa kibali cha polisi au bila kibali cha polisi
mbele ya wajumbe na wageni ambao wengine sio Watanzania,” alisema Omar.
Aliongeza kuwa kauli kama hiyo, haiwezi
kusemwa hata na Rais ambaye ni Amiri Jeshi Mkuu.
Alimtaka Mbowe afahamu dhamana kubwa ya
uongozi aliyonayo kwa wafuasi wake na Watanzania kwa ujumla, wakimtaka afuate
misingi ya sheria za nchi, katiba na utawala bora.
Pia, alisema kauli zilizotolewa na Mbowe,
hazibebeki na mtu yeyote katika taifa hili, kwani alitoa kauli mbaya kuliko
zote kisiasa, ambazo zimewahi kusemwa majukwaani.
“Watanzania tukikaa bila kuzilaani na
kuzikemea kauli zake tutakuwa hatujitendei haki sisi wenyewe na pia
hatuvitendei haki vizazi vijzvyo vya nchi yetu,” aliongeza.
Alihoji uhalali wa kutoa amri hizo kwa
wafuasi wake, ilhali ni kiongozi tu wa chama, tena ambacho hakiko madarakani.
Alisema Watanzania wanapaswa kuwakataa
viongozi wenye jazba na kutumia mabavu katika kutimiza majukumu yao, kwani
wanaweza kuiingiza nchi katika vurugu zisizo na ulazima.
Pia alivitaka vyombo vya dola,
visizivumilie kauli kama hizo, zilizotolewa na Mbowe, kwani vyombo vya dola
vina dhamana ya kulinda, kutunza na kuendeleza amani na utulivu wa nchini,
wachukue hatua kali za kisheria kwa kauli ya kutishia uvunjifu wa amani kabla
hajaingiza nchi kwenye machafuko ya kisiasa.
Wakati
huo huo, viongozi wa juu wa chama hicho, leo wamepanga kumsindikiza Mbowe
kwenda Makao Makuu ya Jeshi la Polisi nchini, ambako ameitwa kwa barua.
Katibu
Mkuu wa chama hicho, Dk Willibrod Slaa alisema Mbowe alipokea barua, ikimtaka
afike Makako Makuu ya jeshi hilo leo saa 5:00 asubuhi.
“Mwenyekiti
wetu ameitwa Makao Makuu ya Polisi leo na hatujui kaitiwa nini, huenda
anakwenda kuhojiwa na huenda mwito huo umetokana na kauli alizotoa awali katika mkutano mkuu, ambazo
zililenga kuhamasisha maandamano ya nchi nzima kupinga Bunge la Katiba linaloendelea”,
alisema Dk Slaa.
Alitaja
watakaoongoza msafara wa amani wa kumsindikiza Mbowe kuwa ni mwanasheria wao, mbunge wa Singida Mashariki,
Tundu Lissu, Makamu Mwenyekiti wa Chadema (Bara), Profesa Abdallah Safari na
Mwanasheria Peter
Kibatala.
Hata
hivyo, alisema pamoja na kiongozi huyo kuitwa na polisi, bado jeshi hilo
haliwezi kuvunja ajenda ya kuandamana, kwa kuwa ilipitishwa na Kamati Kuu ya
chama hicho, na kwamba polisi wao wanapaswa kutoa kibali cha kuruhusu
maandamano hayo.
Awali,
alisema maazimio yaliyopitishwa na
Kamati Kuu ya chama hicho ni kuunganisha nguvu ya pamoja na vyama
vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) .
Alisema
maazimio hayo, yataanza Desemba 14, mwaka huu, siku ambayo uchaguzi wa serikali
za mitaa unaanza.
Alieleza
kwamba chama hicho kimeunda kamati ya watu watano, itakayoangalia jinsi
ushirikiano wa Ukawa utakavyokuwa kwenye uchaguzi huo.
Hata
hivyo, alisisitiza kuwa kutoka kwao nje bungeni, kulikuwa sahihi. Alisema
katiba mpya, haiwezi kupatikana leo au kesho.
No comments:
Post a Comment