Rais
Jakaya Kikwete, amefanya ziara ya kushtukiza katika maeneo kunakofanyika
maandalizi ya kukinga nchi dhidi ya maambukizi ya virusi vinavyosababisha homa
hatari ya ebola, ikiwemo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere
(JNIA), Dar es Salaam.
Akizungumza
katika ziara hiyo jana, Rais Kikwete alisema
ameshitukiza makusudi na aliipanga juzi usiku na kuianza jana asubuhi,
ili ajionee mwenyewe hatua zilizochukuliwa dhidi ya ugonjwa huo.
"Nimeamua
kuja mwenyewe kuona, msikute mnanilisha maneno tu ya uongo kuhusu hatua
zinazochukuliwa katika hadhari dhidi ya ebola, sasa nimeona na ninachoomba
tumieni pia fursa hii kuboresha," alisema Rais Kikwete ambaye ziara yake
ilianzia JNIA na kufuatiwa na Kituo Maalumu Tengefu katika Hospitali ya Wilaya
ya Temeke.
Mara tu
baada ya kutua JNIA, Dar es Salaam, akitokea Dodoma, Rais Kikwete alikwenda moja kwa moja kukagua
vifaa, huduma na maandalizi ya jinsi Tanzania inavyojiandaa kubaini na
kushughulikia wagonjwa wa ebola, ambao wanaweza kupitia kwenye uwanja huo.
Rais
Kikwete alioneshwa kamera na mashine za kuchanganua picha (Scanners), ambazo
tayari zimefungwa kwenye eneo ambalo abiria hulitumia kuingilia katika uwanja
huo.Baada ya ukaguzi huo, alitoa
angalizo kwamba hadhari hiyo dhidi ya ebola ifanyike kwa makini, ili
isilete shida ya utaratibu kwa wageni na wenyeji wanaoingia au kutoka ndani ya
nchi, hususan kupitia viwanja vya ndege.
“Ugonjwa
huo usiwe kikwazo kwa abiria kupita kwenye uwanja wetu huu. Tutengeneze mfumo
na utaratibu unaowezesha wasafiri kupita katika eneo hilo kama ambavyo imekuwa
siku zote, lakini wakati huo huo mashine zetu zikiwa tayari kugundua haraka ni
msafiri yupi ana matatizo ama dalili za ugonjwa huo.
“Tusitengeneze
mfumo unaozalisha msongamano ndani ya uwanja wa ndege. Napenda kuona wasafiri
wanaendelea kuutumia uwanja wetu, bila msongamano na ucheleweshwaji wowote.
Abiria wasipate taabu kwa sababu ya ebola,” alisema Rais Kikwete.
Baada
ya kumaliza ukaguzi wake katika Uwanja wa Ndege, Rais Kikwete alikwenda moja
kwa moja katika Kituo Kikuu cha Kutenga na Kuhudumia Wagonjwa wa Ebola katika
Mkoa wa Dar es Salaam, katika Hospitali ya Wilaya ya Temeke.
“Nimeanzia
Uwanja wa Ndege. Nia yangu ni kuona utayari wetu katika kukabiliana na ugonjwa
hatari wa ebola, kuona jinsi gani mifumo yetu inavyofanya kazi, kwa ujumla
wake, kukabiliana na janga hili hatari sana,” alisema Rais Kikwete ambaye
alifuatana na Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid na Mkuu wa Mkoa
wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadik.
Baada
ya kushuhudia maandalizi ya kituo hicho, Rais Kikwete alisema hakina hadhi
nzuri na kinahitaji ukarabati zaidi kwani awali majengo hayo yalitengwa kwa
ajili ya wagonjwa wa kipindupindu.
"Pamoja
na hatua mlizochukua za kutenga kituo hiki kuwa cha wagonjwa wa ebola, lakini
bado kina upungufu, kwa sababu kilikuwa cha wagonjwa wa kipindupindu na pia
kiko karibu na makazi, kingetakiwa kiwe mbali, ila paboresheni pawe pa kisasa
kwa hadhi ya nyakati za leo.
“Nataka
kuona kituo chenye viwango vya kuhudumia watu wa tamaduni zote na watu wa hadhi
zote, kuanzia aliyevaa lubega hadi kwa yule mwenye suti ya sehemu tatu…tena
wekeni sehemu ya kupika chakula kwa ajili ya wagonjwa,” alisema Rais Kikwete.
Akijibu
hoja hiyo ya Rais, Mratibu wa Huduma za Dharura Mkoa wa Dar es Salaam, Dk
Christopher Mnzava, alisema wameshaomba fedha Hazina Sh milioni 500, fedha
ambazo wanazingoja ili kukamilisha ukarabati unaohitajika.
Katika
kituo hicho, Rais Kikwete alielezwa kuwa kila mgonjwa mmoja wa ebola ataweza
kuhudumiwa na wafanyakazi wanne wa sekta ya afya, ambapo nguo na magauni yao
yatachomwa moto kila watakapomaliza kumhudumia mgonjwa.
Pia
alielezwa kuwa tayari wanataaluma 1,200 wamepewa mafunzo ya kuhudumia mgonjwa
wa ebola katika Mkoa wa Dar es Salaam na vifaa vyenye thamani ya Sh milioni 119
vimenunuliwa.
Mbali
na maandalizi hayo, daktari mmoja ametumwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
(DRC), kupata uzoefu wa kukabiliana na ugonjwa huo.
Waziri
Rashid naye alimwambia Rais Kikwete kuwa kitaifa maandalizi yanaendelea na
mpaka jana, ‘Scanners’ tayari zilikuwa
zimeshafungwa katika viwanja vya ndege vya Dar es Salaam, Zanzibar, Kilimanjaro
na Mwanza na katika vituo vya mipaka ya Tanzania
na nchi za Uganda, Rwanda, Burundi na Zambia.
Alisema
pia maagizo yametolewa kwa hospitali zote nchini kuwa na vyumba maalumu vya
kuwatenga na kuwahudumia wagonjwa wa ebola.
Wiki
iliyopita, akizungumza na viongozi na wazee wa Mkoa wa Dodoma kwenye Ukumbi wa
Mikutano wa Chuo cha Mipango, Rais
Kikwete ambaye alikuwa amemaliza ziara ya mkoa huo, alizungumzia tishio la
ugonjwa huo na hatua zinazochukuliwa na Serikali kukabiliana nalo.
No comments:
Post a Comment