HOSPITALI YA AGA KHAN KUCHUNGUZA SARATANI YA MATITI



Hospitali ya Aga Khan Dar es Salaam, imezindua kampeni ya kupambana na saratani ya matiti iliyopewa jina la 'Fanya Sasa, Usisubiri mpaka Oktoba' yenye lengo la kukuza ufahamu juu ya umuhimu wa kufanyiwa uchunguzi mapema.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Daktari Bingwa wa Upasuaji, Aidan Njau alisema kuwa kampeni hiyo imelenga kupiga vita ugonjwa huo ambao umekuwa ni tatizo kubwa nchini.
Alisema kila Jumamosi ya kwanza ya mwezi, hospitali hiyo itakuwa ikifanya kliniki ya bure ya uchunguzi wa saratani ya matiti na kutoa elimu lengo likiwa ni kuwahamasisha watu wapime afya zao haraka badala ya kusubiri mpaka mwezi Oktoba ambao unajulikana kama mwezi wa saratani ya matiti.
Alisema ili hatua hiyo ilete tija, lazima uchunguzi ugundue saratani kabla ya dalili kujionesha ambazo humlazimu mtu kutafuta huduma hospitalini.
Alizitaja sababu zinazoweza kusababisha hatari ya kupata saratani kuwa ni  historia ya nyuma juu ya familia, mifumo ya maisha ikiwemo uvutaji wa sigara, aina za vyakula na historia ya maambukizi ya virusi na saratani mtu aliyokuwa nayo kwa kipindi cha nyuma.

No comments: