Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid Mohamed (CUF) ametangaza
kugombea urais wa Zanzibar huku
akimtuhumu na kumkosoa Katibu Mkuu wa chama chake, Seif Hamad.
Alitumia jukwaa la
Bunge Maalum la Katiba kumshambulia Seif
ambaye ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, akisema ni kiongozi mwenye
lengo la kuvunja muungano.
Baada ya Mwenyekiti, Samuel Sitta kumpa fursa ya kuzungumza,
mbunge huyo alisema anatumia nafasi hiyo
kumjibu Seif, ambaye juzi alirushwa na
kituo kimoja televisheni, akitoa tuhuma
mbalimbali kwake kuhusu yeye kubaki bungeni na kamati namba tano aliyokuwa
anaiongoza.
Hamad alisema Seif ametoa shutuma nyingi za uongo dhidi
yake, kwa sababu amepata taarifa kuwa yeye Hamad ana nia ya kugombea urais wa Zanzibar na hilo kwake limekuwa tatizo
kubwa.
“Nilitaka kugombea ukatibu mkuu ukanitimua, sasa huna nafasi
ya kunitimua ninapoenda kugombea urais, na kweli nagombea urais. Nilikuwa
sijasema naenda kugombea wapi, leo nasema naenda kugombea Zanzibar…asiingiwe na
kiwewe,” alisema Hamad Rashid huku akishangiliwa na wajumbe wenzake.
Hamad alisema atagombea urais kama mgombea binafsi, kama
itakubalika kwenye Katiba, lakini kama hilo litakataliwa, atagombea urais wa
Zanzibar kupitia chama ambacho yeye ni mshauri wake cha Alliance For Democracy Change (ADC).
Kuhusu madai kwamba
amebaki bungeni kwa sababu ana uchu wa madaraka, Hamad alisema “Mimi sijagombea mara nne urais, wala
sijawahi kutoka makamu mwenyekiti wa chama nikawa katibu mkuu na nikarudi tena
kuwa makamu wa chama halafu nikarudi tena kuwa katibu mkuu wa chama sijawahi.”
Hamad alisema Seif ni kiongozi ambaye anatakiwa kuwa wazi na
sio kuwa na sura mbili, kwani anawayumbisha watu. Alihoji, “Kiongozi kama huyo
akiwa amri jeshi mkuu mwenye sura mbili si jeshi lote litapigwa kwa sababu
atakuwa anawayumbisha watu.”
Akijibu tuhuma mbalimbali, ikiwemo ya kwamba Hamad yuko
bungeni kwa sababu ya upendeleo anaofanyiwa na spika wa Bunge, Anna Makinda
kwani kesi aliyoifungua mahakamani ilikwishaisha, Hamad alisema kesi hiyo
haijaisha na itaendelea kusikilizwa tena Septemba 26 mwaka huu.
Hamad alisema Makinda
alikuwa makini katika kushughulikia suala lake la kuvuliwa uanachama, kwani
hakutaka kuingilia masuala ya mahakama, bali aliiachia mahakama itoe uamuzi
wake na yeye atafanya uamuzi wa kisheria.
“Kwa hiyo kumpandikizia lawama spika, sio jambo jema, ni
vyema Maalim Seif amwombe radhi ” alisema Hamad.
No comments:
Post a Comment