Aliyekuwa
Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona (73) ameieleza Mahakama kuwa, Benki
Kuu (BoT) ilihusika kusimamia mchakato
wa kutafuta kampuni ya kukagua uzalishaji wa dhahabu nchini kwa njia ya zabuni.
Yona alidai
hayo jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakati akijitetea dhidi ya
tuhuma za matumizi mabaya ya madaraka na kuisababishia serikali hasara ya Sh
bilioni 11.7.
Akiongozwa na
Wakili wake, Elias Msuya, Yona alidai, waliamua kutafuta kampuni ya kukagua
uzalishaji wa dhahabu kutokana na malalamiko ya wananchi na taasisi mbalimbali
wakidai kuna tatizo katika Sekta ya Madini.
Alidai wizara
yake pamoja na BoT ambayo ilikuwa inasimamia akaunti za kampuni za nje
zinazochimba madini nchini, walikubaliana watafute mkaguzi wa uzalishaji wa
dhahabu, afanye kazi ya kufuatilia madini yanayochimbwa, gharama na kiasi gani
yanauzwa nje ya nchi.
Aliongeza
kuwa waliamua BoT ndiyo isimamie mchakato wa kumpata Mkaguzi huyo kwa njia ya
zabuni kwa kuwa ndiyo inahusika na utaratibu wa malipo na inasimamia akaunti za
makampuni hayo.
Alidai Machi
3, 2003 alimwandikia Rais barua kumweleza kuhusu mapendekezo yao ya kumpata
Mkaguzi wa Madini, Machi 20, Rais
alikubali ombi lao na kuwataka waendelee na mchakato huo haraka.
Alidai baada
ya kupata kibali cha Rais waliendelea na mchakato huo wakishirikiana na Wizara
ya Fedha pamoja na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu (AG).
Mei 20, 2003, alimwandikia tena Rais barua kumueleza majadiliano kati ya wizara yake, Wizara ya
Fedha na BoT yanaendelea vizuri.
Yona alidai,
Gavana wa BoT aliandaa Kamati ya kupata Mkaguzi huyo, wizara yake ikiwakilishwa
na Godwine Nyelo na wawakilishi wengine kutoka Wizara ya Fedha na Ofisi ya AG.
Alidai
Novemba 27, 2003, Nyelo alimpa taarifa kuwa wameshampata Mkaguzi huyo lakini
hajui walitumia njia gani kumfikishia taarifa mzabuni. Kesi hiyo imeahirishwa
hadi leo Yona atakapoendelea kujitetea.
Washitakiwa
wengine katika kesi hiyo ni aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba na Katibu
Mkuu wa zamani wa Wizara ya Mipango na Uchumi, Gray Mgonja.
Wanadaiwa
kati ya Agosti mwaka 2002 na Juni 14, 2004 jijini Dar es Salaam, wakiwa
watumishi wa umma, walitumia vibaya madaraka yao na kuisababishia serikali hasara
ya Sh bilioni 11.7.
Ilidaiwa
walisababisha hasara hiyo baada ya kutoa msamaha wa kodi kinyume cha sheria kwa
Kampuni ya M/S Alex Stewart ya nchini Uingereza.
No comments:
Post a Comment