WAVUVI 9 WAFARIKI DUNIA ZIWA TANGANYIKA

Wavuvi tisa wakazi wa kijiji cha uvuvi cha Mpasa wilayani Nkasi mkoa wa Rukwa, wamekufa baada ya boti waliyokuwa wakisafiria kuzama katika Ziwa Tanganyika.
Habari kutoka eneo la tukio,  ambazo pia zimethibitishwa na jeshi la polisi, zinasema wavuvi  hao walikuwa  wakisafiri kwenda  katika Mji wa Mpulungu, mwambao mwa Ziwa  Tanganyika katika nchi jirani ya Zanmbia. Walikuwa  wakitokea kijiji cha uvuvi  cha Mpasa  wilayani Nkasi.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Ferdinand  Rwegasira,  alithibitisha kutokea  kwa ajali hiyo. Alisema  miili  yote  tisa  ya waliokuwa wakisafiri ndani ya boti  hiyo, haijapatikana  hadi sasa.
Alitaja wanaosadikiwa  kufa ni Fadhili Nkambi (30), Shaaban Kasokota ((33) Audifas Miele (43), Linus Maliyatabu (38), Kashindi Tantika (25), Venus Albeto (35), Geofrey Kazumba (24), Mwambe Ntapantapa (21) na Mathias Ulaya (20) .
Kamanda Rwegasira  alisema uchunguzi  wa ajali hiyo  ya majini,  bado unaendelea na  pia wanaendelea kutafuta miili  hiyo.
Akizungumza na mwandishi kwa simu kutokea  eneo la tukio, Ofisa Mtendaji  wa Kata ya Kasanga  mwambao  mwa Ziwa Tanganyika  wilayani Kalambo, Francis Simfukwe  alisema wavuvi  hao  walianza safari  yao kuelekea Zambia Julai 28 mwaka huu  sasa 11:00 alfajiri .
Alisema  wavuvi hao  walikuwa  wakisafiri kwenda mji wa Mpulungu, Zambia  kuuza samaki  wao,  waliowavua  kwa ndoano na kuwahifadhi katika  makasha  27, ambapo  kila mvuvi alikuwa na makasha  matatu .
“Sasa kwa kuwa walikuwa wakikwepa kupitia  kijijini  Kasanga  ili wasiweze kulipa  ushuru wa samaki hao,  waliokuwa wakisafirishwa  kwenda  nchi jirani ya Zambia,    walipita  nchi jirani ya  Kongo ( DRC)  katika  Ziwa,  hivyo kufanikiwa  kukwepa  kupita  katika kijiji cha Kasanga  ambayo ni bandari  ya mwisho  katika Ziwa Tanganyika  kwa upande wa Tanzania  kabla ya  kuingia  nchini  Zambia,”  alidai Simfukwe.
Kwa mujibu  wa Simfukwe,  wavuvi  hao  walipofika  vijiji vya uvuvi  vya Kilewani na Kipwa  mwambao  mwa Ziwa Tanganyika  wilayani Kalambo,  ghafla  upepo mkali ulivuma  ndipo walipoamua  kuanza kurejea ufukweni  mwa  kijiji cha uvuvi  cha Kipwa. Lakini,  boti yao  ilipigwa na dhoruba kali na kuzama.
“Siku iliyofuata  makasha  manne yakiwa na samaki  wabichi,  huku yakiwa  yameandikwa  majina,  yalionekana  yakielea ziwani  katika kijiji cha Kipwa…ndipo tulipohisi kuwa  kuna ajali  imetokea  ziwani," alieleza Simfukwe.
Simfukwe alisema wakazi wa kijiji  cha  uvuvi  cha Nsumba mwambao mwa Ziwa Tanganyika  nchini Zambia,  walitoa  taarifa kuwa wameona mtumbwi  ukielea  ziwani, karibu na kijijini chao ukiwa  hauna wala mashine ya  kuendeshea.
Baadhi ya  wavuvi  wa kijiji cha Mpasa,  walimweleza mwandishi wa habari  hizi  kwa njia ya simu,  kwa masharti ya kutoandikwa  majina yao, kuwa  baada ya  kukatika kwa mawasiliano ya  simu  baina  yao  na wavuvi wenzao, waliokuwa  wakisafiri  kwa boti kuelekea  nchini Zambia kuuza  samaki wabichi,  walianza  kuwatafuta .

No comments: