'WANAWAKE DUNIANI KOTE HAWAPENDI VITA'


Mke wa Waziri Mkuu, Tunu Pinda amesema wanawake wote duniani hawapendi vita wala machafuko na hulilia amani kwani machafuko husababisha kutoweka kwa amani kuanzia ngazi ya familia na kuleta  vifo vya watu wasio na hatia.
 Alisema hayo jana wakati akitoa mada akiwa mzungumzaji mkuu kwenye Mkutano wa Dunia wa siku tano unaofanyika Seoul, Korea Kusini unaojadili masuala ya amani, usalama na maendeleo.  
Mkutano huo umeandaliwa na Taasisi ya Universal Peace Federation (UPF) ambayo
hutoa ushauri kwenye Baraza la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia masuala ya Uchumi na Kijamii.
Akiwasilisha mada kuhusu usalama, amani na maendeleo barani Afrika, Mama Tunu
alisema “Ninaiomba jamii ya kimataifa duniani kote tusimamie amani na usalama
kwani kinyume na hapo ni kuleta machafuko na vita… wanawake hatupendi vita wala machafuko.”  
Aliwataka washiriki wa mkutano huo kusimama katika nafasi zao kama wazazi na vijana na kuhakikisha dunia inakuwa ni mahali pazuri pa kuishi.
“Ninawasihi tuendeleze maono ya Muumba wetu, tuweke utu mbele kwa kuwajali wengine na tuache kutanguliza maslahi yetu binafsi,” alisema Mama Pinda. 
Mapema, akiwakaribisha wajumbe zaidi ya 500 kutoka nchi 68 wanaoshiriki mkutano huo, Rais wa UPF, Dk Thomas Walsh alisema taasisi hiyo inasimamia misingi ya amani, usalama na maendeleo ya jamii kwa nia ya kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa mataifa mbalimbali.
Alisema katika mkutano huo anatarajia ushiriki wa wakuu wa nchi mbalimbali na viongozi mashuhuri, ambao utasaidia kupata majibu ya changamoto inayoikabili dunia juu ya upatikanaji wa amani ya kudumu. 
Kwa upande wake, Mfalme Letsie Mswati III wa Lesotho, akizungumza katika mkutano huo alisema dunia inakabiliwa na changamoto nyingi za ukosefu wa amani kubwa ikiwa ni uharibifu wa mazingira.
Aliwataka wajumbe wa mkutano huo kuhakikisha wanahimiza utunzaji wa mazingira kama njia ya kupunguza matatizo yanayojitokeza kutokana na mabadiliko ya tabianchi.
Kadhalika alionya kwamba kuna haja ya kuweka mifumo madhubuti ya kuhakikisha kuwa dunia haiendelei kuwa na matukio ya kigaidi na matumizi ya silaha za maangamizi.
“Kama tutakubali vita viendelee kutokea, na migogoro isiyokwisha barani Afrika na nchi za Uarabuni, ni lazima tukubali kuwa hakutakuwa na maendeleo katika mabara
haya,” alisema.

No comments: