TANZANIA KUUNDA JESHI LA KULINDA AMANI AFRIKA

Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) limeendelea kung’ara kimataifa, ambapo jana jeshi hilo lilitamkwa kuwa miongoni mwa majeshi ya nchi za Afrika, yatakayounda Jeshi la Kulinda Amani Afrika.
Taarifa za ndani kutoka Mkutano wa Kimataifa wa Wakuu wa Nchi na Serikali zaidi ya 50 za Afrika na Marekani, ambao umehudhuriwa pia na Rais Jakaya Kikwete, zimeeleza kuwa moja ya kazi za jeshi hilo, itakuwa kuwa tayari wakati wowote, kukabiliana na tishio la kiusalama ndani ya Afrika.
Taarifa za Shirika la kimataifa la habari la Reuters, zilizotolewa jana, zilieleza kuwa Serikali ya Marekani katika mkutano huo uliomalizika juzi, imejipanga kutumia Dola za Marekani milioni 110 kila mwaka kwa miaka mitatu mpaka mitano ijayo, kusaidia jeshi hilo kufanya kazi kwa haraka katika maeneo yanayokabiliwa na tishio la usalama na amani Afrika.
Hivi karibuni vikao vya JWTZ vinavyolinda amani Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), vilitajwa kuwa miongoni mwa vikosi bora 35 vya majeshi ya nchi mbalimbali duniani, vinavyokubalika kwa kuwa na ufanisi wa hali ya juu, uwezo mkubwa wa kupigana na vilivyofundishwa vizuri.
Mtandao wa Kimataifa wa Imgur Via Distractify, ulieleza kuwa Tanzania ni nchi pekee ya Afrika,  yenye jeshi ambalo ni miongoni mwa majeshi bora 35 duniani.
Mwandishi, Micky Wren aliandika katika mtandao huo kuwa,  majeshi hayo, ikiwemo JWTZ yamefundishwa kwa kiwango cha juu, yana silaha za kisasa na yameandaliwa vizuri kwa ajili ya operesheni ngumu za kijeshi.
Pia, majeshi hayo yalitajwa kuwa yenye uwezo wa kukabiliana na adui katika mazingira yoyote, kuanzia kumaliza uhuni wa utekaji  hadi kusambaratisha wahalifu wenye uwezo mkubwa.
Mwandishi huyo alitaja majeshi hayo katika orodha ambayo haikupangwa kwa mtitiriko wa uwezo wa kijeshi, ambapo mbali na JWTZ mengine ni Kikosi cha Seal cha Jeshi la Maji la Marekani na Kikosi cha SAS cha Jeshi la Uingereza.
Kipo pia Kikosi cha Huntsmen Corps cha Majeshi Maalumu ya Denmark, Majeshi Maalumu ya Ufaransa, Kikosi cha MARSOC, Majeshi Maalumu ya Taiwan ambayo yanatumia kinga za usoni zisizoweza kuingiliwa na risasi na Kikosi cha Irish Army Rangers cha Jamhuri ya Ireland.
Vingine ni Gendarmerie cha Serbia, Kikosi Maalumu cha Kukabiliana na Ugaidi cha JTF2 cha Canada, Majeshi Maalumu ya Uholanzi, Kikosi cha SBS, Majeshi Maalumu ya Jamhuri ya Korea na Majeshi Maalumu ya Ufaransa.
Pia, yapo Majeshi Maalumu ya Ubelgiji, Kikosi cha MJK cha Norway, Canadian Joint Response Unit cha Canada, Majeshi Maalumu ya Norway, Kikosi cha French Commando Marine, Majeshi Maalumu ya New Zealand, Kikosi cha Norwegian Armed Forces Special Command na Kikosi cha Polish Grom cha Poland.
Vingine ni Kikosi cha US Army Special Forces Sniper with Remington Modular Sniper Rifle, Majeshi Maalumu ya Marekani, Majeshi Maalum ya Indonesia, Majeshi Maalum ya Romania na Kikosi cha SASR cha Australia.
Kikosi cha KSK cha Ujerumani, Majeshi Maalumu ya Ujerumani, Majeshi Maalumu ya Israel – Shayetet 13, Majeshi Maalumu ya Urusi – Spetsnaz, Majeshi Maalum ya Austria – Jagdkommando, Majeshi Maalumu ya Iraq, Majeshi Maalumu ya Ujerumani ya SEK-M na Majeshi Maalumu ya Peru.
Maofisa wa Serikali ya Marekani, wamekaririwa na Reuters wakieleza kwamba mbali na Tanzania, majeshi mengine yatakayounda jeshi hilo yanatoka nchi za Senegal, Ghana, Ethiopia, Rwanda na Uganda.
“Tumeshuhudia kwa muda mrefu sasa majeshi ya nchi za Afrika, yakifanya kazi kwa weledi katika maeneo yenye migogoro,” ilisema Reuters  ikimkariri ofisa mmoja wa Serikali ya Marekani.
Ofisa huyo alisema pamoja na mafanikio ya majeshi hayo ya Afrika, bado kumeendelea kujitokeza changamoto ya kusaidia vikosi vya majeshi hayo, kuingilia kati sehemu zenye migogoro kwa haraka zaidi, pamoja na namna ya kujilinda na kujikimu wakiwa katika majukumu hayo ya kimataifa.
Kutokana na changamoto hizo, fedha hizo zinazofikia Dola milioni 550 baada ya miaka hiyo mitano, zinatarajiwa kuanza kutolewa mwanzoni mwa mwaka wa fedha wa Marekani unaoanza Oktoba mwaka huu, na zitapelekwa moja kwa moja, kusaidia utendaji wa haraka wa jeshi hilo, katika maeneo yanayokabiliwa na tishio la kuibuka kwa migogoro.

No comments: